Magaidi wa Daesh waamua kujisalimisha Mosul, Iraq baada ya kuzingirwa
Jeshi la Iraq limetangaza habari ya kujisalimisha makumi ya wanachama wa kundi la kigaidi na ukufurishaji la Daesh (ISIS) eneo la magharibi mwa mji wa Mosul, kaskazini mwa nchi hiyo.
Najmu al-Jaburi, kamanda wa operesheni za kuukomboa mji wa Mosul kutoka mikononi mwa genge la kigaidi la Daesh, ametangaza kuwa, makumi ya wanachama wa kundi hilo wamejisalimisha kwa jeshi baada ya kusambaratika sekta ya ulinzi ya magaidi hao huko magharibi mwa Mosul. Al-Jaburi amesema magaidi wengi ama wameangamizwa, kujificha au wamejisalimisha.
Jeshi la Iraq kwa kushirikiana na harakati ya kujitolea ya wananchi ya Hashu sh-Sha'abi, limekuwa likiwazingira magaidi wa Daesh katika maeneo ya magharibi mwa Mosul kwa siku kadhaa sasa. Hivi karibuni pia, Waziri Mkuu wa Iraq, Haider al-Abadi alitoa ujumbe kwenda kwa mabaki ya wanachama wa kundi hilo la kigaidi linalopata misaada kutoka Marekani, Israel na baadhi ya nchi za Mashariki ya Kati hususan Saudia, akiwataka ama kujisalimisha kwa jeshi na kuhukumiwa au kuangamizwa.
Wakati huo huo, jeshi la Iraq limetangaza leo kwamba, limefanikiwa kumtia mbaroni kiongozi wa Idara ya Utawala ya kundi hilo.
Habari zinaeleza kuwa, magaidi wa Daesh wamejifisha katika ngome chache zilizosalia ambazo jeshi la Iraq linaendelea kuzikaribia kwa ajili ya kuzidhibiti na kufunga jalada la genge hilo. Hatua ya pili ya operesheni ya kuyakomboa maeneo ya magharibi mwa Mosul, ilianza tarehe 19 mwezi Februari kwa amri ya Waziri Mkuu wa Iraq, Haider al-Abadi.