Safari ya Waziri wa Ulinzi wa Uingereza nchini Saudia
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i34673-safari_ya_waziri_wa_ulinzi_wa_uingereza_nchini_saudia
Jumanne iliyopita, Michael Cathel Fallon, Waziri wa Ulinzi wa Uingereza sambamba na kukutana mjini Jeddah na Mohammad bin Salman bin Abdulaziz Al Saud, Mrithi wa Kiti cha Ufalme nchini Saudia, walitiliana saini mikataba ya ushirikiano wa kiulinzi na kiusalama.
(last modified 2026-01-14T08:12:18+00:00 )
Sep 22, 2017 00:54 UTC
  • Safari ya Waziri wa Ulinzi wa Uingereza nchini Saudia

Jumanne iliyopita, Michael Cathel Fallon, Waziri wa Ulinzi wa Uingereza sambamba na kukutana mjini Jeddah na Mohammad bin Salman bin Abdulaziz Al Saud, Mrithi wa Kiti cha Ufalme nchini Saudia, walitiliana saini mikataba ya ushirikiano wa kiulinzi na kiusalama.

Katika kikao hicho pande mbili zilijadili ushirikiano wa pamoja wa kijeshi na kiusalama na matukio yanayojiri katika eneo la Mashariki ya Kati na kile kilichosemwa kuwa ni juhudi kwa ajili ya kupambana na ugaidi. Katika kipindi cha hivi karibuni, viongozi wa ngazi za juu wa Uingereza akiwemo Theresa May, Waziri Mkuu wa nchi hiyo wamefanya safari mara kadhaa katika nchi za kusini mwa Ghuba ya Uajemi ikiwemo Saudia. Safari hizo zinazofanyika kwa madhumuni ya kuinua kiwango cha mahusiano na nchi hizo zenye utajiri wa mafuta, pia zimelenga kujinufaisha zaidi kiuchumi na kibiashara sambamba na kutiliana saini mikataba ya silaha za mabilioni ya Dola. Aidha mikataba hiyo inakusudia kuongeza uwepo wa kijeshi wa askari wa Uingereza katika eneo la kistratijia la Ghuba ya Uajemi.

Theressa May alipoenda Saudia na kukutana na mwanamfalme Muhammad Bin Salman

Uingereza katika kuendeleza siasa zake na kuongeza kiwango cha uwepo wake hususan katika uga wa kijeshi katika eneo la hili, mwezi Novemba mwaka jana ilifungua kambi ya kijeshi nchini Bahrain, na hivi karibuni pia viongozi wa London wamekithirisha safari zao nchini Kuwait, Qatar, Saudian na Oman kwa lengo la kupanua kiwango cha ushirikiano na kadhalika mauziano ya silaha na nchi hizo za Kiarabu. Ni kwa kuzingatia kuwa Saudia inahesabika kuwa nchi kubwa na muhimu kati ya nchi wanachama wa Baraza la Ushirikiano la Ghuba ya Uajemi, ndio maana katika miaka ya hivi karibuni London imekuwa ikiipa umuhimu mkubwa Riyaddh kwa kuongeza idadi ya mikataba ya kijeshi na silaha na nchi hiyo. Hakuna shaka kwamba, hatua hiyo inatekelezwa kwa malengo makuu mawili.

Silaha haramu za Uingereza zinazotumiwa na Saudia nchini Yemen

Katika sehemu ya kwanza ni kwamba hivi sasa serikali ya Theresa May, inakabiliwa na tatizo la kuzorota sekta ya utengenezaji silaha ambalo limepelekea maelfu ya raia wa nchi hiyo kukosa ajira. Ni kwa ajili hiyo ndio maana imeamua kuongeza kiwango cha mauzo yake ya silaha ili kutatua tatizo hilo. Ni wazi kuwa sehemu kubwa ya silaha hizo zinatumika katika kukandamiza harakati za malalamiko ya wananchi katika nchi hizo za Kiarabu hususan Saudia. Ni kwa kuzingatia ukweli huo ndipo nchi hizo za Magharibi hususan Uingereza, zikawa zinafumbia macho ukiukaji wa wazi wa haki za binaadamu unaoshuhudiwa nchini Saudia, bali zinashiriki pia katika jinai na maafa makubwa yanayotekelezwa na utawala wa Aal-Saud katika mashambulizi ya kinyama ya miezi 30 sasa nchini Yemen.

Silaha za Uingereza ambazo zinawaua watoto wa Yemen

Kwa hakika Saudia ni mnunuzi mkubwa wa zana za kijeshi za Uingereza ambapo hadi sasa mikataba ya mauziano ya silaha na zana za kijeshi kati ya nchi mbili tangu mwaka 2015 imekaribia kiasi cha dola bilioni nne. Kwa mujibu wa Sergey Syberibov, mtaalamu wa masuala ya kisiasa wa nchini Russia, Marekani na Uingereza zinapata faida kubwa kupitia vita vya Saudia nchini Yemen. Kwa mujibu wa uchunguzi mpya uliofanywa na taasisi ya 'Uungaji Mkono kwa Watoto wa Vita ya Uingereza-War Child UK', mashirika makubwa ya silaha nchini Uingereza yametuhumiwa kupata faida kubwa kutokana na mauaji yanayofanywa na Saudia dhidi ya watoto wasio na hatia wa nchi za Kiarabu na hasa wa Yemen kupitia mauzo ya silaha na makombora kwa nchi za Ghuba ya Uajemi hususan Saudi Arabia. Kuhusiana na suala hilo Rocco Bloom, mshauri wa shirika la misaada ya kibinaadamu nchini Uingereza anasema: "London imeingia katika kashfa ya ukiukaji wa haki za binaadamu, kutokana na hatua yake ya kushindwa kuwalinda watoto wasio na hatia wa Yemen, Syria na Iraq kupitia biashara yake ya mauzo ya silaha." Mwisho wa kunukuu.

Aghlabu ya silaha zinazotumiwa na magaidi duniani zinatoka Uingereza na Marekani

Suala hilo linabainisha undumakuwili wa madola ya Magharibi kuhusiana na madai yao ya kuheshimu haki za binaadamu. Serikali ya kihafidhina ya Uingereza licha ya kutolewa ripoti tofauti na mashirika ya haki za binaadamu kuhusiana na mauaji ya halaiki yanayofanywa na Saudia dhidi ya raia wa kawaida wa Yemen na kadhalika mashambulizi ya ndege za kivita za nchi hiyo na washirika wake dhidi ya maeneo na maeneo ya kiraia ya taifa hilo la Kiarabu (Yemen) sambamba na malalamiko ya kila mara ya walimwengu kuhusiana na ukiukwaji wa haki za binaadamu wa Riyadh, bado London imeendelea kuimarisha mahusiano yake na utawala wa Aal-Saud. Kwa msingi huo, safari ya Michael Cathel Fallon, Waziri wa Ulinzi wa Uingereza nchini Saudia na utilianaji saini wa mikataba mipya ya ushirikiano wa kiulinzi na usalama kati ya Riyadh na London, kunamuondolea shaka mtu yeyote kuhusiana na ushirikiano wa kiwango cha juu wa nchi hizo katika mauaji ya halaiki ya watoto, wanawake na wazee wa Yemen, Syria na Iraq.