Jan 08, 2020 02:48 UTC
  • Middle East Eye: Saudia inazidisha mashaka ya Waislamu wa Rohingya

Kituo cha habari cha Middle East Eye kimeripoti kuwa, Saudi Arabia inazidisha mashaka na masaibu ya Waislamu wa jamii ya Rohingya huko Myanmar kwa kuwasaka, kuwakamata na kuwafukuza Warohingya wanaofanya kazi nchini humo.

Middle East Eye imesema Waislamu wa jamii ya Rohingya waliokuwa wakifanya kazi nchini Saudi Arabia na kutuma baadhi ya kipato chao kwa familia zao zilizofukuzwa Myanmar na kuishi kwenye kambi za wakimbizi nchini Bangladesh sasa wanakamatwa na kutumuliwa nchini humo kutokana na kile kinachoitwa marekebisho ya mrithi wa ufalme wa nchi hiyo, Muhammad bin Salman.

Muhammad Faroq aliyekuwa akifanya kazi nchini Saudia anasimulia jinsi askari usalama wa nchi hiyo walivyomkamata na kumfunga katika kituo cha al Shumaisi chenye idadi kubwa ya Waislamu wa Rohingya waliotiwa nguvuni na utawala wa Saudia wakisubiri kufukuzwa nchini humo.saudia

Wahajiri wa Kirohingya wanakamatwa na kunyanyaswa Saudia

Anasema yanayofanyika nchini Saudia dhidi ya Waislamu wa Rohingya wanaofanyakazi nchini humo ni kielelezo cha ukosefu wa rehma na huruma.

Maafa hayo ya Waislamu wa Rohingya huko Saudia ambao wamefukuzwa nchini kwao kutokana na mauaji na ukatili wa kutisha wa jeshi na mabudha wa Myanmar yamepingwa vikali na taasisi za kutetea haki za binadamu.

Itakumbukwa kwamba Umoja wa Mataifa umesema kuwa kinachofanyika nchini Myanmar dhidi ya Waislamu wa Rohingya ni mauaji ya kimbari.

Maelfu ya Waislamu hao wameuawa na wengine karibu milioni moja wamekimbilia katika nchi jirani hususan Bangladesh wakihofia maisha yao.  

 

 

 

Tags