Feb 23, 2021 06:41 UTC
  • Israel yawakamata viongozi kadhaa wa HAMAS na mateka Wapalestina walioachiwa huru

Utawala haramu wa Kizayuni wa Israel umewatia nguvuni viongozi kadhaa wa Harakati ya Muqawama wa Kiislamu ya Palestina HAMAS katika maeneo ya Ufukwe wa Magharibi wa Mto Jordan na Baitul Muqaddas pamoja na mateka Wapalestina waliochiwa huru.

Klabu ya mateka Wapalestina imeeleza katika taarifa kwamba adui Mzayuni amevamia nyumba za Wapalestina katika Ufukwe wa Magharibi na Quds na kuwatia nguvuni Wapalestina 20 wakiwemo wanachama waandamizi wa Hamas na mateka Wapalestina walioachiwa huru na kuwakabidhi kwa vyombo vya usalama vya utawala huo ghasibu.

Katika kamatakamata hiyo iliyofanyika jana, askari wa jeshi la utawala wa Kizayuni wamevamia pia nyumba ya Mustafa Ash-Shanar na kumtia nguvuni mkuu huyo wa chuo kikuu cha An-Najah kilichoko katika mji wa Nablus.

Asakri katili wa Israel baada ya kumkamata kijana wa Kipalestina

Askari wa Kizayuni wanavamia nyumba na kuwatia nguvuni hata mateka Wapalestina walioachiwa huru wakati Serikali ya Mamlaka ya Ndani ya Palestina imetangaza kuwa itawasilisha ombi rasmi kwa utawala haramu wa Israel la kuutaka uwaruhusu mateka Wapalestina wanaoshikliwa kwenye jela za utawala huo washiriki katika zoezi la upigaji kura la uchaguzi wa bunge la Palestina.

Kwa mujibu wa tangazo lililotolewa na Rais Mahmoud Abbas wa Mamlaka ya Ndani uchaguzi wa bunge la Palestina utafanyika tarehe 22 Mei na ule wa rais wa mamlaka hiyo utafanyika tarehe 31 Julai mwaka huu na kwamba endapo uchaguzi wa bunge hautaingia katika duru ya pili, uchaguzi wa bunge la taifa la Palestina utafanyika tarehe 31 Agosti.../

Tags