Njama za UNICEF za "kurubuni" watoto wa Yemen zagunduliwa al Hudaydah
(last modified Mon, 03 May 2021 07:50:40 GMT )
May 03, 2021 07:50 UTC
  • Njama za UNICEF za

Maafisa wa Yemen katika mkoa wa al Hudaydah wamegundua shehena iliyotumwa na Shirika la Kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa (UNICEF) kama zawadi kwa waototo wa Yemen ambayo ina mifuko ya shule na ramani zinazoutambua rasmi utawala haramu wa Israel badala ya Palestina.

Ripoti kutoka Yemen zinasema kuwa, maafisa wa mkoa wa al Hudaydah wametangaza kuwa, UNICEF ilikuwa na nia ya kusambaza mifuko na ramani hizo baina ya watoto wa shule katika mkoa huo lakini shehena hiyo imegunduliwa na kukamatwa na polisi maafisa usalama. 

Jabir al Razihi ambaye ni miongoni mwa maafisa wa serikali katika mkoa wa al Hudaydah amesema, hii si mara ya kwanza kukamatwa shehena ya bidhaa kama hizo na kuongeza kuwa, harakati kama hizi zinazofanywa na taasisi na mashirika ya kimataifa chini ya mwavuli wa misaada ya kibinadamu kwa taifa la Yemen, ni katika mikakati ya maadui ya kuhudumia maslahi ya Marekani na utawala wa Kizayuni wa Israel.

Al Razihi ameongeza kuwa, harakati hizo hatari na za kihasama za mashirika kama UNICEF ni katika jitihada za kusambaza fikra ya kutambuliwa rasmi utawala haramu wa Israel baina ya watoto wa Yemen na vizazi vijavyo. 

Njama hiyo imegunduliwa huku Waislamu katika maeneo mbalimbali ya dunia wakijitayarisha kwa ajili ya maandamano ya Siku ya Kimataifa ya Quds iliyotangazwa na hayati Imam Ruhullah Khomeini kwa ajili ya kutetea Msikiti wa al Aqsa, (kibla cha kwanza cha Waislamu), na ardhi tukufu ya Palestina.

Maandamano ya Siku ya Kimataifa ya Quds hufanyika kila mwaka katika Ijumaa ya mwisho ya mwezi mtukufu wa Ramadhani.