Ripoti: Israel imewakamata Wapalestina 1,900 tangu mwanzo wa 2021
Tangu mwanzo wa mwaka huu wa 2021, Utawala wa Kizayuni wa Israeli umewakamata Wapalestina wasiopungua 1,900, pamoja na idadi kubwa ya watoto, kote katika mji wa al-Quds (Jerusalem) unaokaliwa kwa mabavu na utawala huo.
Vyombo vya habari vikinukuu harakati za kutetea haki za Wapalestina ziliripoti Jumapili kwamba kukamatwa kwa watu wengi kulifanywa kufuatia Operesheni ya ‘Upanga wa al-Quds’. Hii ilikuwa oparesheni ya mwezi Mei ya makundi ya kupigania ukombozi wa Palestina ambayo ilitikelezwa kujibu jinai za utawala wa Kizayuni wa Israel. Katika oparesheni hiyo makundi ya kupigania ukombozi wa Palestina yalivurumisha maelfu ya makombora ndani ya Israel na kuwaangamiza Wazayuni wasiopungua 12 mbali na kusababisha hasara kubwa.
Klabu ya Wafungwa wa Palestina ilisema kwamba utawala wa Israeli ulikuwa umewashikilia hasa vijana ili kuwatia hofu na kuwazuia kukabiliana na vikosi vyake.
"Kukamatwa kulilenga sana watoto walio chini ya umri wa miaka 18, kwa lengo la kuwavunja moyo wasikabiliane na askari wa Israel, ” imesema ripoti hiyo.
Kwa ujumla hivi sasa kuna wafungwa zaidi ya 4,600 Wapalestina wanaoshikiliwa katika magereza ya kuogofya ya Israel.
Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) imekuwa ikiwateka nyara Waisraeli ili kuushinikiza utawala haramu wa Israel uwaachilie huru wafungwa Wapalestina.
Mwaka 2011, utawala wa Kizayuni wa Israel ulilazimika kuwaachilia huru wafungwa 1,000 Wapalestina, akiwemo kiongozi wa sasa wa Hamas Yahya Sinwar, mkabala wa kuachiliwa huru Gilad Shalit, mwanajeshi wa Israel ambaye alikuwa ameshikiliwa mateka Ghaza kwa zaidi ya miaka mitano.