Saudia yawaua wanajeshi wa Hadi mkoani Shabwah, Yemen
Muungano vamizi wa kijeshi wa Saudi Arabia na Imarati umeua wanajeshi kadhaa wa rais wa zamani wa Yemen aliyejiuzulu na kutoroka nchi, Abdu Rabbuh Mansour Hadi.
Duru za kiusalama zinaarifu kuwa, wanajeshi 15 wa Mansour Hadi wameuawa katika shambulizi la anga la muungano huo wa kijeshi katika wilaya ya Al-Makha katika mkoa wa Shabwah.
Habari zaidi zinasema kuwa, askari wengine sita wamejeruhiwa vibaya katika hujuma hiyo iliyolenga makao makuu ya mamluki wa Saudi Arabia na Imarati katika mkoa wa Shabwah.
Inaarifiwa kuwa, kambi hiyo imesambaratishwa kikamilifu katika shambulio hilo, ambalo muungano vamizi wa Saudia unadai kuwa limefanyika kimakosa.
Ifahamike kuwa, mkoa wa Shabwah upo chini ya udhibiti wa Umoja wa Falme za Kiarabu, na vikosi vitiifu kwa serikali iliyojiuzulu ya Mansour Hadi.
Hivi karibuni, Abdul Aziz Jabbari, Naibu Spika wa kile kinachoitwa Bunge la Wawakilishi huko kusini mwa Yemen alifichua kuwa, licha ya Mansour Hadi kujikomba na kujitweza kwa Saudi Arabia na Imarati, lakini watawala wa Riyadh na Abu Dhabi wamekataa kumruhusu mwanasiasa huyo mwenye umri wa miaka 76 kulihami na kulizatiti kwa silaha jeshi lake.