Miaka arubaini baada ya jinai ya Israel ya Sabra na Shatila
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i88260-miaka_arubaini_baada_ya_jinai_ya_israel_ya_sabra_na_shatila
Septemba 16, inasadifiana na kumbukumbu ya miaka 40 ya jinai iliyotekelezwa na utawala haramu wa Israel huko Sabra na Shatila nchini Lebanon .
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Sep 17, 2022 06:29 UTC
  • Miaka arubaini baada ya jinai ya Israel ya Sabra na Shatila

Septemba 16, inasadifiana na kumbukumbu ya miaka 40 ya jinai iliyotekelezwa na utawala haramu wa Israel huko Sabra na Shatila nchini Lebanon .

Kuanzia tarehe 16 hadi 18 Septemba 1982 utawala wa Kizayuni wa Israel uliizingira kambi ya Sabra na Shatila iliyoko magharibi mwa Beirut na kuwaua kwa umati wanawake, watoto na wazee wa Kipalestina 3,500 na idadi kadhaa ya Walebanon kwa muda wa siku tatu.

Miaka ya 1980 ni muongo ambapo utawala wa Kizayuni wa Israel unaokalia Quds Tukufu (Jerusalem) kwa mabavu ulifanya uhalifu mkubwa zaidi dhidi ya Walebanon. Kwa hakika, katika kipindi cha muongo huo, Lebanon ilikuwa kitovu cha jinai za Wazayuni. Vita na mauaji ya raia vilijumuishwa katika ajenda ya utawala huo. Wakati huo huo, wakimbizi wa Kipalestina na raia wa Lebanon pia walilengwa na Wazayuni watenda jinai. Jinai hizo za utawala wa Kizayuni wa Israel zina nukta kadhaa za uchambuzi wa kisiasa ndani yake.

Nukta ya kwanza ni kwamba, jinai ya Sabra na Shatila ilithibitisha wazi kwamba utawala katili wa Israel umeegemea kwenye misingi ya ubaguzi wa rangi, ugaidi na kuwaangamiza  raia wasio na hatia wakiwemo  wakimbizi. Nasser Kanani, Msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameandika katika ukurasa wake wa Instagram kwa mnasaba wa kukumbuka mwaka wa 40 wa jinai za askari wa utawala wa Kizayuni katika kambi za wakimbizi wa Palestina huko Sabra na Shatila kwamba:  “Mwa huu, tarehe 16 Septemba, inasadifiana na miaka arubaini tangu kuanza kwa ukatili wa siku 3 wa mauaji ya kutisha na yasiyofikirika yaliyotekelezwa dhidi ya wakimbizi wa Kipalestina katika kambi hizo.

Sabra na Shatila kusini mwa Beirut zilikuwa mikononi mwa utawala huo wa Kizayuni wa kigaidi na waitifaki wake. Huu haukuwa uhalifu wa kwanza wa utawala huu bandia, wala haukuwa wa mwisho. Msingi wa utawala wa kibaguzi wa Kizayuni umejikita katika uchokozi, jinai na ukiukwaji wa wazi wa sheria za kimataifa na haki za binadamu na daima utatishia amani na usalama wa kimataifa.

Nukta ya pili ni kwamba, Wazayuni daima wamekuwa wakitumia fursa ya usaliti wa baadhi ya makundi katika nchi za Kiislamu, na usaliti ni miongoni mwa sifa za kisiasa katika baadhi  nchi za Kiislamu. Uhalifu wa Sabra na Shatila pia ulifanywa kwa usaliti wa kundi la Falanga la Samir Geagea huko Lebanon. Nyaraka zilizotolewa hivi majuzi na ofisi ya Waziri Mkuu wa Israel Yair Lapid pia zinathibitisha usaliti wa wanamgambo hao wanaoshirikiana na Geagea. Katika nyaraka hizo, uhusiano wa moja kwa moja kati ya shirika la kijasusi la Israel (Mossad) na kundi la Falanga la Lebanon umefichuliwa. Imeelezwa katika hati hizo kwamba wakuu wa utawala bandia wa Israel walisema mwanzoni mwa miaka ya 1980 kwamba, “tuna wafuasi nchini Lebanon ambao ni mali yetu”. Hata hivi leo Wazayuni katika nchi tofauti za Kiislamu wanafaidika na usaliti wa baadhi ya watu na makundi ambayo hulinda maslahi yao.

Jinai ya Sabra na Shatila iliyongozwa na Ariel Sharon (kulia) wakati akiwa waziri wa vita wa Israel

Nukta ya tatu ni kuwa, kuibuka muqawama au harakati ya mapambano ya Kiislamu nchini Lebanon yaani Hizbullah ndio uliokuwa mwisho wa kukaliwa kwa mabavu nchi hiyo na utawala wa Kizayuni, jambo ambalo lilifanyika taratibu, na hivi leo vikosi vya muqawama vinatetea mamlaka na mipaka yote ya ardhi ya Lebanon. Suala hili pia ni sababu kuu ya uhasama dhidi ya Hizbullah hasa kutoka Marekani na baadhi ya makundi ya ndani ya Lebanon. Harakati ya Hizbullah imefanikiwa kufunga njia zote za usaliti uliokuwepo miaka ya nyuma ingawa bado kuna wale wanaoendelea kuuza nchi yao.

Nukta ya nne ni kuwa, jinai ya Sabra na Shatila sawa na jinai nyingine zilizotendwa na utawala katili  wa Israel haijaweza kukabiliwa na adhabu yoyote kutoka jamii ya kimataifa, na utawala huo umeweza kukwepa mkono wa sheria kufuatia jinai zake hizo kutokana na uungaji mkono wa madola ya Magharibi hususan Marekani.