Mark Carney: Canada haitasahau usaliti wa Marekani/ Mahusiano ya zamani yamekwisha
(last modified Tue, 29 Apr 2025 12:01:36 GMT )
Apr 29, 2025 12:01 UTC
  • Mark Carney
    Mark Carney

Waziri Mkuu mteule wa Canada, Mark Carney ametoa ujumbe mzito kwa Marekani, akisema kwamba Ottawa haipaswi "kusahau usaliti wa Washington ambao umeathiri vibaya uhusiano wa kibiashara wa nchi hizo mbili.

Carney amesema haya leo Jumanne baada ya chama chake cha Liberal kushinda viti vingi vya uwakilishi bungeni huku kukiwa na mvutano unaoongezeka kati ya Canada na serikali ya  Rais wa Marekani, Donald Trump kuhusu sera za biashara.

"Tutashinda vita hivi vya kibiashara," Waziri Mkuu mteule wa Canada amewaambia wafuasi wake mjini Ottawa na kutahadharisha kuhusu changamoto zinazoikabili nchi hiyo kutokana na sera za ushuru na vitisho ya Trump. 

Mark Carney ameeleza wazi katika hotuba yake baada ya kuibuka mshindi kwamba uhusiano wa jadi kati ya Canada na Marekani umebadilika. Aidha amesisitiza kuwa mfumo wa biashara huria ya kimataifa ulioimarishwa na Marekani, mfumo ambao Canada imekuwa ikiutegemea tangu Vita vya Pili vya Dunia, umekwisha.

Mvutano kati ya nchi hizo mbili unaendelea kuongezeka, hasa baada ya Marekani kutangaza ushuru wa asilimia 25 kwa magari yanayotengenezwa Canada.

Ushuru uliotangazwa na Trump hasa ongezeko ambalo limeathiri biashara ya magari yanayotengenezwa Canada umeathiri vibaya uchumi wa nchi hiyo na aghalabu ya Wacanada wanazitaja hatua hizo za Rais wa Marekani kuwa ni dharau kwa mamlaka ya kujitawala ya Canada.