Joe Biden: Trump atimuliwe kutoka White House
Joe Biden, mgombea aliye na nafasi nzuri ya kushinda uchaguzi wa awali ndani ya chama cha Democrat nchini Marekani kuelekea uchaguzi wa rais wa 2020, ametaka Rais Donald Trump wa nchi hiyo atimuliwe kutoka ikulu ya White House.
Biden ameyasema hayo leo kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Facebook ambapo ameandika kwamba: "Trump amevunja mkataba wa mazingira na kutishia usalama wa mustakbali wa dunia, hivyo ni lazima tumuondoe kutoka White House." Aidha Joe Biden ambaye alikuwa makamu wa rais wa Barack Obama ameongeza kwamba, Marekani inahitaji rais ambaye hatoshusha hadhi yake kufikia kiwango cha kushambuliana binafsi na wenzake na badala yake awaunganishe Wamarekani.
Kwa sasa Biden anaonekana kuwa mshindani mkubwa wa Rais Donald Trump ambapo kwa mujibu wa kura ya maoni, kuna uwezekano mkubwa akawa mgombea mkuu wa chama cha Democrat dhidi ya Trump kwenye uchaguzi wa mwakani. Aidha tangu Trump alipoingia madarakani amekuwa akimshambulia vikali Joe Biden kutokana na wasi wasi wake wa kuchuana naye kwenye uchaguzi wa 2020 ambapo katika uwanja huo amewahi kumtaja kwa jina la 'Joe Msinziaji.'