Mripuko wa ugonjwa wa surua waua watoto 74 Afghanistan
Mripuko wa ugonjwa wa surua (measles) umeua makumi ya watoto kaskazini mwa Afghanistan.
Maazudin Ahmadi, Mkuu wa Ofisi ya Habari na Utamaduni katika mkoa wa Badakhshan kaskazini mwa Afghanistan amesema mlipuko huo wa surua umeua watoto wasiopungua 74.
Amesema maambukizi ya maradhi hayo yameripotiwa katika wilaya za Kuf Ab, Darwaz, Kohistan vilevile makao makuu ya mkoa huo, Faizabad.
Afisa huyo wa mkoa wa Badakhshan kaskazini mwa Afghanistan amesema akthari ya watoto hao walioaga dunia kwa ugonjwa wa ukambi walikuwa wanaishi katika maeneo yasiyo na maafisa wala vituo vya afya.
Afghanistan inakabiliwa na matatizo chungu nzima, kuanzia migogoro ya kiafya, kiuchumi na kiusalama. Zaidi ya watu milioni 22 nchini Afghanistan wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula.
Aidha taarifa ya hivi karibuni ya Shirika la Kazi Duniani (ILO) ilieleza kuwa zaidi ya nusu ya wananchi wa Afghanistan wamepoteza ajira zao katika miezi ya karibuni na kwamba mwenendo huo umeisababisha jamii ya nchi hiyo matatizo mengi.