Aug 11, 2016 01:33 UTC
  • Alhamisi,  Agosti 11,  2016

Leo ni Akhamisi tarehe 8 Dhilqaada 1437 Hijria inayosadifiana na tarehe 11 Agosti 2016.

Tarehe 11 Oktoba miaka 487 iliyopita Martin Luther alitangaza rasmi madhehebu ya Protestant. Uprotestanti ulianzishwa na Martin Luther kama harakati ya kidini katika karne ya 16 kwenye ulimwengu wa Kikristo kwa lengo la kufanya mageuzi ya kidini. Harakati hiyo ilianza dhidi ya kanisa Katoliki na udikteta wa viongozi wa madhehebu hiyo kuhusu suala la msamaha wa dhambi unaotolewa na makasisi na Papa. Martin Luther aliyekuwa Mjerumani alianza harakati hiyo ya uasi ndani ya kanisa Katoliki baada ya kufasiri Injili kwa lugha ya Kijerumani tofauti kabisa na amri ya Papa kwa lengo la kuvunjilia mbali taasubu za kimadhehebu za Kikatoliki.

Siku kama ya leo miaka 64 iliyopita inayosadifiana na tarehe 11, Agosti 1952 Haile Selassie, mtawala wa Ethiopia alitia saini azimio la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lililokuwa na lengo la kuiunganisha Eritrea na Ethiopia. Ardhi ya Waislamu ya Eritrea ambayo hapo kabla ilikuwa ikikoloniwa na Italia, katika Vita vya Pili vya Dunia ilikaliwa kwa mabavu na Uingereza. Mwezi Disemba 1950 Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa liliidhinisha Eritrea kuongozwa kwa mfumo wa shirikisho sambamba na kuunganishwa na Ethiopia. Hata hivyo kutokana na kwamba wananchi wengi wa Eritrea hawakuridhishwa na hatua hiyo pamoja na kupuuzwa haki zao na utawala wa Ethiopia, walizidisha upinzani wao dhidi ya utawala wa Addis Ababa na hatimaye kuanzisha harakati ya kupigania uhuru wa nchi yao mnamo mwaka 1960. Mwaka 1993 mapambano ya wananchi wa Eritrea yalizaa matunda ambapo walishiriki katika kura ya maoni ya kujitenga na Ethiopia. Eritrea ambayo iko katika eneo muhimu la kiistratijia la kaskazini mashariki mwa bara la Afrika na pwani ya Bahari Nyekundu, inapakana na nchi za Ethiopia, Sudan na Djibouti.

Mtawala wa Ethiopia wa wakati huo Haile Selassie

Siku kama ya leo miaka 56 iliyopita, inayosadifiana na tarehe 11 Agosti 1960  nchi ya Chad ilijipatia uhuru wake kutoka kwa mkoloni Mfaransa na siku hii hutambuliwa kama siku ya kitaifa nchini humo. Mwishoni mwa karne ya 19 na mwanzoni mwa karne ya 20 wakoloni wa Ufaransa waliishambulia Chad na katika kipindi cha miaka mitatu wakaidhibiti ardhi yote ya nchi hiyo. Mwaka 1958 Ufaransa iliipa Chad hiari ya kujiongoza, na miaka miwili baadaye na katika siku kama ya leo, nchi hiyo ikapata uhuru kamili na kuchagua mfumo wa uongozi wa jamhuri. Nchi ya Chad inapakana na nchi za Libya, Cameroon, Sudan, Afrika ya Kati, Nigeria na Niger.

Na siku kama ya leo miaka 7 iliyopita mwafaka na tarehe 11 Agosti 2009 ilianza duru ya sita ya vita kati ya jeshi la Yemen na Mashia wa Zaidia katika milima ya kaskazini mwa nchini hiyo na karibu na mpaka wa Saudi Arabia. Kundi hilo la wanamapambano wa Kishia linajulikana kwa jina la al Houthi, ambalo ni jina la kiongozi wa harakati hiyo. Wapiganaji hao wanataka kuondolewa ubaguzi wa kiuchumi na kitamaduni katika maeneo yao sambamba na kupunguzwa satua na kiwango cha uhusiano wa nchi yao na Marekani. Pamoja na kwamba vita kati ya jeshi la Yemen na Mashia vilianza mwaka 2004, lakini duru ya sita ya vita hivyo ndiyo iliyokuwa kali na kuchukua muda mrefu zaidi. Katika vita hivyo vikosi vya anga vya Saudi Arabia vilivisaidia vikosi vya Yemen katika kuyashambulia maeneo ya Mashia. Aidha katika vita hivyo mamia ya Mashia wa Yemen waliuawa na karibu watu laki mbili kulazimika kuwa wakimbizi.