Darul-Iftaa Misri: Dini zote ziungane kupambana na makundi ya kigaidi
Kituo cha kupambana na misimamo mikali cha Darul-Iftaa nchini Misri kimetangaza kuwa, kuna ulazima wa dini zote za mbinguni kuungana kukabiliana na jinai zinazofanywa na makundi ya kigaidi.
Taarifa iliyotolewa na kituo hicho sambamba na kulaani shambulizi la kigaidi lililofanywa na magaidi katika kituo cha upekuzi cha jeshi la nchi hiyo eneo la Sinai, kimesisitiza kuwa serikali zote za dunia lazima ziungane kupambana na wimbi la makundi ya kigaidi na kufurutu ada. Taarifa hiyo imeongeza kuwa, haifai serikali hizo kutoa mwanya kwa makundi hayo yanayotumia vibaya dini tukufu ya Kiislamu kutenda jinai na uhalifu.
Kituo hicho cha Darul-Iftaa nchini Misri kimefafanua kuwa, dini zote za mbinguni zinalaani jinai kama vile mauaji ya binaadamu wasio na hatia. Kimeongeza kuwa, kundi la kigaidi na kitakfiri la Daesh na mengine kama hilo yanafanya jinai katika nchi tofauti na kwamba njia pekee ya kukabiliana na jinai za magenge hayo ni kuungana pamoja dunia na kuyashinda makundi hayo potofu.
Mripuko wa bomu la kutegwa ndani ya gari uliotokea karibu na kituo cha upekuzi cha jeshi la Misri katika Peninsula ya Sinai, ulisababisha mauaji ya askari 11 wa nchi hiyo. Kundi la kigaidi la Wilayat Sina lililotangaza utiifu wake kwa kundi la kitakfiri la Daesh limetangaza kuhusika kwake katika hujuma hiyo.