Watunisia wataka kuanzishwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi yao na Syria
Makundi ya kiraia nchini Tunisia yametaka kuanzishwa mahusiano ya kidiplomasia baina ya nchi yao na serikali ya Syria.
Makundi hayo ya kiraia sambamba na kufanya sherehe za kufurahia ushindi wa jeshi la serikali ya Syria mjini Tunis, mji mkuu wa nchi hiyo, yameitaka serikali kuanzisha haraka uhusiano wa kidiplomasia na serikali ya Damascus. Katika sherehe hiyo Mubarakah al-Barahimi, mwakilishi wa harakati ya wananchi katika bunge la Tunisia amesema kuwa, kukombolewa miji muhimu ya Syria na jeshi la serikali kwa kushirikiana na muqawama, ni suala lililowaletea furaha kubwa Watunisia wote.
Kwa upande wake Shawqi Rajih, Mjumbe wa jumuiya ya Wasyria yenye makao yake Tunisia amesema kuwa, umefika muda wa kuanzishwa uhusiano baina ya Tunis na Damascus, kwani mataifa ya Tunisia na Syria ni ndugu na ni suala la kawaida mataifa rafiki kufanya mahusiano. Miaka mitano iliyopita, madola ya Kiarabu yaliilazimisha Tunisia kuwa mwenyekiti wa kikao cha nchi zilizo dhidi ya serikali ya Syria.
Hata hivyo licha ya nchi hizo kuiwekea vikwazo vya kisiasa na kiuchumi serikali halali ya Damascus, vikwazo hivyo havijafikia malengo yake hasa baada ya Tunisia kupinga vikali mwenendo huo. Aidha kwa mara kadhaa Watunisia wamefanya maandamano wakilaani uingiliaji wa Saudi Arabia na Qatar kwa uungaji mkono wa Marekani na utawala haramu wa Kizayuni wa Israel huko nchini Syria.