Aboul Gheit: Ni baidi Misri kutumia nguvu za kijeshi dhidi ya Ethiopia
Katibu Mkuu wa Arab League Ahmed Aboul Gheit amesema kuwa, ni baidi Misri kutumia nguvu za kijeshi dhidi ya Ethiopia kuhusiana na tofauti za nchi mbili juu ya ujenzi wa bwawa la al-Nahdha (Renaissance) katika mto Nile.
Gazeti la Saudia la Asharq Al-Awsat linalochapishwa mjini London, Uingereza limemnukuu Aboul Gheit akisema kuwa, suala la kujaza kwa muda mrefu maji ya bwawa la al-Nahdha la Ethiopia kwa kutumia maji ya Mto Nile, linazuia maji ya mto huo kuingia nchini Misri. Amesema kuwa, kujaza bwawa hilo kwa maji ya Mto Nile kutakakochukua kipindi cha miaka 10, kutainyima Misri mita za ujazo bilioni mbili za maji katika sehemu yake ya kila mwaka katika maji ya Mto Nile ambayo kwa kila mwaka ni mita za ujazo bilioni hamsini na tano.
Itakumbukwa kuwa mwaka 2013 serikali ya Ethiopia ilianza kubadili mwelekeo wa mkondo wa maji ya mto huo kwa ajili ya kuandaa uwanja wa ujenzi wa bwawa la al-Nahdha (Renaissance) kwa lengo la kuzalisha umeme. Hatua hiyo iliibua hasira na wasi wasi wa viongozi na wananchi wa Misri kutokana na kupungua maji ya mto Nile na taathira yake mbaya kwa uwezo wa uzalishaji umeme kwenye bwawa la 'al Aal' la Misri.