Wasudan wapinga kutumwa askari wa nchi hiyo kuua watu wa Yemen
Wananchi na vyama vingi vya siasa nchini Sudan vimepinga na kulaani hatua ya serikali ya nchi hiyo ya kutuma kundi jingine la askari wa nchi hiyo kwa ajili ya kushirikiana na wavamizi wa Saudi Arabia na washirika wake wanaoendelea kuua watu wa Yemen.
Vyama vya upinzani nchini Sudan vimetangaza kuwa, nchi hiyo haipati faida yoyote kwa kushiriki katika muungano wa Saudi Arabia dhidi ya watu wa Yemen licha ya kwamba haina sababu ya kushiriki kwenye vita hivyo. Vyama hivyo vimesema askari wa Sudan wanauawa bure katika vita vya Yemen ambavyo vinaendelea kulaaniwa na jamii ya kimataifa.
Vyama vya upinzani nchini Sudan vimeongeza kuwa, hatua ya kutuma askari wa Sudan katika vita vya Yemen imechukuliwa kinyume cha sheria na inachochea chuki ya walimwengu hususan Waislamu dhidi ya watu wa Sudan kwa kushirikiana na Saudi Arabia kuua watu wasio na hatia wa Yemen. Vyama hivyo vimesisitiza kuwa, uamuzi wa serikali ya Sudan wa kutuma majeshi huko Yemen unapingana na matakwa ya wananchi.
Uvamizi na mashambulizi yanayofanywa na Saudi Arabia ikishirikiana na nchi nyingine kadhaa za Kiarabu pamoja na Marekani na utawala haramu wa Israel yameua maelfu ya watu wasio na hatia wa Yemen na kuwalazimisha mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi.