Amnesty yalaani kukingiwa kifua wauaji wa raia Rabi'a al-Adawiyya, Misri
-
maiti za watu waliouawa Rabi'a al-Adawiyya mjini Cairo tarehe 14 Agosti mwaka 2013
Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International limetoa wito wa kufikishwa mahakamani maafisa na watu wote waliohusika na mauaji ya raia katika Medani ya Rabi'a al-Adawiyya katika mji mkuu wa Misri, Cairo.
Taarifa iliyotolewa na Amnesty International imelaani kitendo cha kutofikishwa mahakamani maafisa na watu wote waliohusika na mauaji ya watu katika Medeni ya Rabi'a al-Adawiyya na kusema kuwa, katika ukandamizaji huo uliofanywa dhidi ya watu waliokuwa wakifanya mgomo katika medani hiyo watu wasiopungua 900 waliuawa na maelfu ya wengine kujeruhiwa.
Taarifa hiyo ya Amnesty International imetolewa kwa mnasaba wa kukumbuka mauaji hayo na ukandamizaji wa raia waliokuwa wakifanya mgomo katika Medani ya Rabi'a al-Adawiyya mjini Cairo tarehe 14 Agosti mwaka 2013. Raia hao walikuwa wakipinga hatua ya jeshi la Misri ya kumuondoa madarakani Muhammad Mursi aliyechaguliwa kwa njia za kidemokrasia kuwa rais wa nchi hiyo.
Wamisri wanayatambua mauaji ya Medani ya Rabi'a al-Adawiyya kuwa ndiyo makubwa zaidi katika historia ya sasa ya nchi hiyo.
Amnesty International inasema, hadi sasa hakuna afisa yeyote aliyechukuliwa hatua kutokana na mauaji hayo ya Rabi'a al-Adawiyya.