Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran yuko safarini Afrika Kusini
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Mohammad Javad Zarif leo amewasili Afrika Kusini katika safari yake ya kuzitimbelea nchi kadhaa za bara Afrika.
Zarif yuko safarini katika mji wa Pretoria Afrika Kusini kufuatia mwaliko wa mwenzake wa nchi hiyo Maite Nkoana-Mashabane.
Katika safari hiyo kutafanyika kikao cha 13 cha Tume ya Pamoja ya Iran na Afrika Kusini na pia Zarif anatazamiwa kukutana na Rais Jacob Zuma wa nchi hiyo. Kikao hicho kinatazamiwa kujadili utekelezwaji wa makubaliano baina ya nchi mbili.
Kikao cha 12 cha Tume ya Pamoja ya Iran na Afrika Kusini kilifanyika mwaka 2015 wakati wa safari ya Bi. Nkoana-Mashabane mjini Tehran. Iran na Afrika Kusini zina uhusiano mzuri na viongozi wa nchi hizi mbili hutembeleana mara kwa mara.

Baada ya kuondoka Afrika Kusini, Zarif ataelekea nchini Uganda ambapo atashuhudia kuzinduliwa hospitali yenye vitanda 50 ambayo imejengwa na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Baada ya hapo Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran ataelekea Niger kwa lengo la kufanya mazungumzo na maafisa wa ngazi za juu nchini humo.