Nov 21, 2017 14:26 UTC
  • Watu 50 wauawa katika mripuko wa bomu msikitini nchini Nigeria

Kwa akali watu 50 wameuawa katika shambulio la bomu dhidi ya msikiti mmoja ulioko kaskazini mashariki mwa Nigeria.

Msemaji wa Polisi katika jimbo la Adamawa, Othman Abubakar amesema mripuko huo umetokea mapema leo katika mji wa Mubi, wakati Waumini wa Kiislamu walipokuwa wakiingia msikitini hapo kwa ajili ya Sala ya alfajiri.

Amesema kundi la kigaidi na kitakfiri la Boko Haram ndilo limehusika na shambulizi hilo, na kwamba idadi ya watu waliojeruhiwa ni kubwa mno ingawaje hawana takwimu rasmi kwa sasa.

Naye Bayi Muhammad, mmoja wa waumini wanaokwenda katika msikiti huo na ambaye ameshuhudia tukio hilo amesema baadhi ya wahanga wa hujuma hiyo ya kikatili wameteketea kiasi cha kutotambulika.

Baadhi ya wanachama wa kundi la kigaidi la Boko Haram

 

Shambulizi hilo la kigaidi linahesabiwa kuwa mauaji makubwa zaidi ya umati nchini Nigeria mwaka huu.

Haya yanajiri chini ya wiki moja baada ya magaidi wanne wa Boko Haram kujiripua kwa bomu mjini Maiduguri, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo ambapo mbali na watu 18 kuuawa, wengine 30 walijeruhiwa.

Kundi la Boko Haram lilianzisha mashambulizi yake ya kigaidi mwaka 2009 ambapo hadi sasa zaidi ya watu elfu 20 wameuawa nchini Nigeria, Cameroon, Chad na Niger.

Tags