Mkuu wa Baraza la Utawala wa Mpito Sudan ala kiapo
Abdulfattah al Burhan Mkuu wa Baraza la Utawala wa Mpito Sudan ambaye ana jukumu la kukabidhi madaraka kwa serikali ya kiraia amekula kiapo.
Abdulfattah al Burhan ambaye anatazamiwa kukabidhi madaraka kwa serikali ya kiraia kutoka baraza la kijeshi kwa muda wa miaka mitatu amekula kiapo cha uongozi leo Jumatano. Jana Jumanne ilitangazwa kuwa wajumbe wa Baraza la Kijeshi la Sudan na wapinzani wameweza kufikia makubaliano kuhusu muundo wa baraza hilo la la utawala mpito nchini humo litakaloongozwa na wajumbe 11. Makubaliano hayo yanaandaa mazingira ya kufanyika uchaguzi mkuu na kuundwa serikali kwa njia ya kidemokrasia.
Abdallah Hamdok kutoka muungano wa wapinzani Sudan ameteuliwa kuwa Waziri Mkuu na rais wa muda wa serikali hiyo. Sudan imetumbukia kwenye machafuko makubwa katika miezi ya karibuni baada ya kupinduliwa Rais wa nchi hiyo Omar al Bashir.
Sudan aidha imeshuhudia mapigano kati ya wanajeshi na wafanya maandamano. Makubaliano haya kati ya wanajeshi Sudan na wapinzani yameungwa mkono na kukaribishwa pakubwa na taasisi za kimataifa. Umoja wa Afrika pia umeyataja makubaliano hayo kuwa ni ya kihistoria.