Nchi za SADC kutumia satalaiti ya pamoja kwa ajili ya ustawi
Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika SADC imetangaza mpango wa kutuma angani kwa pamoja sataliti ili kuimarisha maendeleleo endelevu barani Afrika.
Hayo yamedokezwa na Waziri wa Mawasiliano ya Simu nchini Angola, Mario Oliveira ambaye amesema, utekelezaji wa mfumo wa kutumia kwa pamoja satelaiti utasaidia nchi za Afrika kupata taarifa haraka na hivyo kuimarisha maendeleo endelevu barani humo.
Akizungumza katika semina ya SADC iliyofanyika mjini Luanda, Oliveira ameongeza kuwa hatua hiyo itakuwa muhimu kwa nchi wanachama wa SADC kuingia kwenye sekta ya anga za mbali.

Naye mratibu wa ngazi ya juu wa sayansi, teknolojia na mawasiliano wa SADC Geoge Ah-Thew amesema, nchi wanachama wa Jumuiya hiyo zinaandaa sera kwa ajili ya mfumo huo wa utumizi wa pamoja wa satalaiti.
Hayo yanajiri wakati ambao nchi zingine za Afrika tayari zimerusha satalaiti katika anga za mbali. Nchi hizo ni pamoja na Afrika Kusini, Nigeria, Misri, Algeria, Kenya, Rwanda, Ghana, Angola, Morocco, Sudan na Ethiopia.