Yumkini idadi ya waliouawa Burundi imepindukia 1,000
Umoja wa Mataifa umetaarifiwa kuwa idadi ya watu waliouawa katika mgogoro wa kisiasa nchini Burundi yumkini imepindukia watu 1,000.
Pierre Claver Mbonimpa, mtetezi wa haki za binadamu nchini Burundi amewaambia waandishi wa habari katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York nchini Marekani kwamba, waliouawa kufikia sasa ni watu 1,098 na kwamba wengine zaidi ya 800 hawajulikani waliko.
Kadhalika mwanaharakati huyo wa Burundi ambaye pia ni Mwenyekiti wa shirika la Human Rights and Incarcerated Persons HRIP ameuambia umoja huo kuwa, zaidi ya watu 5,000 wanazuiliwa katika jela za nchi hiyo na kwamba maafisa wa usalama nchini humo wameshadidisha ukiukaji wa haki za binadamu na haswa kwa wapinzani wa serikali ya Rais Pierre Nkurunziza.
Wakati huo huo, Zeid Ra’ad Al-Hussein, Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa amesema kuwa, watu 31 wameuawa mwezi huu wa Aprili pekee katika machafuko hayo, ukilinganisha na watu tisa mwezi uliopita.
Hii ni katika hali ambayo, serikali ya Bujumbura imesema haitahudhuria mazungumzo ya kuupatia ufumbuzi mzozo huo yanayotazamiwa kufanyika mjini Arusha, Tanzania mapema mwezi ujao.
Kwa mujibu wa takwimu za UN, zaidi ya watu 400 wameuawa na wengine karibu laki mbili na 60 elfu wamekuwa wakimbizi tangu mwezi Aprili mwaka jana, wakati Burundi ilipotumbukia kwenye machafuko yaliyotokana na Rais Nkurunziza kuamua kugombea tena urais kwa muhula wa tatu.