Maelfu waandamana Tunisia kutaka rais Kais Saeid na serikali nzima wajiuzulu
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i89324-maelfu_waandamana_tunisia_kutaka_rais_kais_saeid_na_serikali_nzima_wajiuzulu
Wapinzani na wakosoaji wa rais Kais Saeid wa Tunisia wamefanya maandamano makubwa wakimtaka kiongozi huyo na serikali ya sasa ya nchi hiyo wajiuzulu.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Oct 15, 2022 23:00 UTC
  • Maelfu waandamana Tunisia kutaka rais Kais Saeid na serikali nzima wajiuzulu

Wapinzani na wakosoaji wa rais Kais Saeid wa Tunisia wamefanya maandamano makubwa wakimtaka kiongozi huyo na serikali ya sasa ya nchi hiyo wajiuzulu.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Tasnim, makumi ya maelfu ya waandamanaji na wakosoaji wa Rais Kais Saeid wa Tunisia, jana Jumamosi walimiminika kwenye barabara kuu za mji mkuu wa nchi hiyo Tunisia wakiandamana kumtaka kiongozi huyo na serikali iliyopo wajiuzulu.
Ahmed Najib al-Shabi, kiongozi wa Chama cha Wokovu wa Kitaifa cha Tunisia, ameashiria kura ya maoni ya katiba iliyofanyika hivi karibuni na kueleza kwamba: "kura hii ya maoni ilifanyika sambamba na maandamano makubwa ambayo sisi tuliyaandaa dhidi ya kura hiyo".
Al-Shabi ameongezea kwa kusema: "lengo letu ni kukomesha upinduaji uliofanywa na kurejea kwenye utawala wa sheria wa katiba".
Kiongozi huyo wa Chama cha Wokovu wa Kitaifa cha Tunisia amekosoa utendakazi wa rais wa Tunisia na kusema kuwa amejitenga na yuko peke yake.
Rais Kaid Saeid

Mnamo Julai 25, 2021, Rais wa Kais Saeid, alipitisha maamuzi na kuchukua hatua kadhaa zisizo za kawaida ikiwemo kutangaza kufuta mamlaka ya Bunge, kuondolewa kwa kinga ya wabunge, kumuuzulu waziri mkuu na kuvunja tume ya usimamizi wa katiba, hatua ambazo zilizusha mtafaruku na mkwamo wa kisiasa nchini Tunisia, ambao uliambatana na wimbi la maandamano ya vyama na mirengo ya kisiasa, kikiwemo chama cha Kiislamu cha Ennahda.

Lakini mbali na hatua hizo, Julai 25, 2022, Saeid aliitisha kura ya maoni ya katiba mpya ambayo ilipitishwa licha ya kupigiwa kura na Watunisia wachache.

Wapinzani wanachukulia hatua za Rais wa Tunisia kuwa ni mapinduzi dhidi ya katiba iliyoidhinishwa mwaka 2014 na mabadiliko ya kidemokrasia yaliyopatikana kupitia mapinduzi ya umma ya mwaka 2011 yaliyohitimisha utawala wa kidikteta wa Zine El Abidine Ben Ali, lakini Saied mwenyewe anasisitiza kuwa hatua zake zimelenga kuiokoa Tunisia na msambaratiko wa kiuchumi na kijamii.../