Apr 13, 2024 12:56 UTC
  • IRGC yaikamata meli yenye uhusiano na Israel katika Mlango-Bahari wa Hormuz

Shirika rasmi la habari la Jamhuri ya Kiisamu ya Iran IRNA limeripoti kuwa kikosi maalumu cha wanamaji cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) kimekamata meli ya makontena ya MCS Aries yenye uhusiano na utawala wa Kizayuni wa Israel karibu na Mlango-Bahari wa Hormuz.

Kwa mujibu wa IRNA, meli hiyo imezuiliwa na Kikosi Maalumu cha Wanamaji cha Sepah (SNSF) katika operesheni ya helikopta ya ushushaji askari wa kikosi cha makomandoo kwenye sitaha ya meli.
 
IRNA imeongezea kwa kusema: "meli hiyo sasa imeelekezwa kwenye eneo la maji ya nchi yetu".
 
Meli hiyo yenye bendera ya Ureno inaendeshwa na shirika la Zodiac Maritime, linalomilikiwa na mfanyabiashara wa Kizayuni Eyal Ofer.
 
Zodiac Maritime ni shirika tanzu la Zodiac Group ambalo ni milki ya bilionea huyo Muisraeli.
Meli ya MCS Aries

Mkanda wa video uliotolewa na Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu IRGC unawaonyesha makomandoo wa SNSF wakishuka kwenye rundo la makontena yaliyowekwa kwenye sitaha ya meli hiyo.

Katika mkanda huo wa video, anasikika bahari mmoja wa meli hiyo akisema: “msitoke nje,” kisha anawaambia wenzake waende kwenye eneo la kuendeshea meli huku makomandoo zaidi wa IRGC wakishuka kwenye sitaha.

Ripoti zinasema, taarifa za meli hiyo ya MSC Aries zilipatikana mara ya mwisho karibu na Dubai jana Ijumaa wakati ikielekea Mlango-Bahari wa Hormuz.

Imeelezwa kwamba, meli hiyo ilizima mitambo ya ufuatiliaji wa taarifa zake, ambao ni utaratibu wa kawaida unaotumiwa na meli zenye uhusiano na utawala wa Kizayuni wa Israel zinazopita katika eneo hili la Ghuba ya Uajemi.

Tukio hilo limetokea wakati utawala haramu wa Israel ukiwa umejiweka katika hali ya tahadhari kwa kuhofia ulipizaji kisasi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kufuatia shambulio la kigaidi la Aprili Mosi ulilofanya utawala huo wa Kizayuni kwenye jengo la ubalozi mdogo wa Iran katika mji mkuu wa Syria Damascus, na kusababisha vifo vya washauri saba wa kijeshi wa IRGC wakiwemo majenerali wawili.../

 

Tags