Khatibu wa Swala ya Ijumaa Tehran: Utawala wa Kizayuni umeshindwa huko Gaza
-
Imamu wa Swala ya Ijumaa, Tehran
Khatibu wa Swala ya Ijumaa mjini Tehran amesema: Utawala wa Kizayuni wa Israel haujafanikiwa lolote katika mashambulizi yake huko Gaza isipokuwa kushindwa.
Hujjatul Islam Mohammad Javad Haj Ali Akbari, Khatibu wa Swala ya Ijumaa ya leo mjini Tehran ameashiria jinai na mashambulizi yanayoendelea kufanywa na Israel katika Ukanda wa Gaza na kusema kuwa, katika kipindi chote cha miezi saba na nusu, utawala wa Kizayuni haujapata mafanikio ya maana isipokuwa kushindwa katika diplomasia, kwenye uwanja wa vita na mbele ya maoni ya umma; na kwa upande mwingine, wanamapambano wa Palestina wamepata mafanikio na fahari katika diplomasia, uwanja wa mapambano na katika maoni ya umma.
Khatibu wa Swala ya Ijumaa ya Tehran amesema kuwa, kambi ya Muqawama imetoa pigo kubwa kwa utawala wa Kizayuni wa Israel, na Wazayuni na washirika wao hawaamini kwamba baada ya vita vya miezi saba na nusu, harakati hiyo ya Muqawama ingali katika medani ya vita.
Akigusia jinai zinazofanywa na utawala wa Kizayuni katika Ukanda wa Gaza, Hujjatul Islam Mohammad Javad Haj Ali Akbari amesisitiza kuwa: Israel imenasa katika kinamasi cha kashfa za pande zote.