Jun 30, 2024 02:15 UTC
  • Kazem Gharibabadi: Marekani inaangalia haki za binadamu kwa jicho la utashi wa kisiasa

Katibu wa Baraza la Haki za Binadamu la Iran ameashiria utashi wa kisiasa wa Marekani katika suala la haki za binadamu na kusema kuwa, Washington imevaa vazi la kutetea haki za binadamu lakini kimsingi inalitumia hilo kufikia malengo yake ya kisiasa.

Kazem Gharibabadi amesema kuwa, Marekani ina mtazamo wa kisiasa kabisa kuhusu haki za binadamu na haina imani kabisa na suala la kuheshimu haki za binadamu.

Gharibabadi ameongeza kuwa, moja ya vielelezo vya kuwa ni wa kisiasa mtazamo wa Marekani kuhusiana na suala la haki za binadamu ni kutojali kwake jinai zinazofanywa na utawala wa Kizayuni ni katika Ukanda wa Gaza.

Katibu wa Baraza la Haki za Binadamu la Iran ameeleza kuwa, hujuma na uvamizi wa Marekani katika baadhi ya nchi kama vile Iraq na Afghanistan, ambao ulisababisha vifo vya mamilioni ya watu katika nchi hizo, ni ishara nyingine ya Marekani kulitumia kisiasa suala la haki za binadamu.

Maandamano ya kupinga ukiukaji wa haki za binadamu nchini Marekani unaofanywa na vyombo vya usalama

 

Kadhalika amesema, vikwazo vya kiuchumi vya Marekani dhidi ya mataifa mengine ni kielelezo kingine cha wazi cha Washington kulitumia kisiasa suala la haki za binadamu. Aidha amesema, Marekani imeziwekea vikwazo vya kiuchumi nchi 25, jambo ambalo ni kinyume cha kanuni na sheria za kimataifa za kibinadamu.

Hivi karibuni pia, Gharibabadi alisema bayana kwamba, hatua ya Marekani ya kuunga mkono makundi ya kigaidi hasa yaliyotenda jinai hapa Iran na wakati huo huo kuendelea kuliwekea vikwazo taifa la Iran ni ushahidi wa wazi kwamba, inasema uongo inapodai kwamba, inawaunga mkono wananchi wa Iran.