Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran awaonya maadui, mkijaribu mtashindwa tena
-
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Sayyid Abbas Araghchi
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Sayyid Abbas Araghchi, amezionya Marekani na utawala wa Kizayuni wa Israel kuhusu kuanzisha tena hatua mpya za kijeshi dhidi ya Iran, akisema kuwa makabiliano ya awali yalishindwa kufikia malengo yaliyokusudiwa, na kwamba jaribio lolote la baadaye litapata matokeo yaleyale.
Mwanadiplomasia huyo mkuu alitoa kauli hizo pembeni mwa mkutano wa mawaziri wa mambo ya nje wa nchi wanachama wa BRICS uliofanyika New Delhi siku ya Alhamisi, akijibu vitisho vilivyotolewa na maafisa mbalimbali wa Marekani na Israel.
Araghchi amesema: “Tumezoea vitisho hivi. Kwa muda mrefu wamekuwa wakirudia vitisho vyao kwa namna na sura tofauti. Lakini wao wenyewe pia wanajua kwamba hawakupata chochote, wala hawatapta chochote, kupitia vitisho hivyo au hata kupitia vita walivyoanzisha.”
Ameongeza kuwa: “Natumai wataachana na lugha ya vitisho na kuelekea kwenye mantiki, ingawa matumaini ni madogo kwamba watarejea kwenye busara. Lakini wanapaswa kufahamu kwamba suluhisho la masuala mbalimbali halipatikani vitani, kwa sababu hawatapta matokeo yoyote kupitia njia hiyo.”
Araghchi pia amesema kuwa nafasi ya Iran katika eneo hilo imeimarika kufuatia ushindi dhidi ya washambuliaji. Ameongeza kuwa: “Sasa, mataifa yote yanatambua kwamba Jamhuri ya Kiislamu ndiyo iliyoshinda katika vita hivi na ilifanikiwa kuwazuia maadui wake kufikia malengo yao huku ikilazimisha matakwa yake yenyewe.”
Kwa mujibu wa Araghchi, mijadala katika mkutano wa BRICS imeonyesha kuwepo kwa tathmini mpya ya hali ya kisiasa na kiusalama katika eneo hilo baada ya vita.
Amekumbusha kwamba, kwa hatua ya kujibu mashambulizi dhidi yake, Iran ililenga “ngome za Marekani pekee kwenye ardhi ya Umoja wa Falme za Kiarabu.”
Waziri huyo wa mambo ya nje pia alitoa wito wa kuwa na mtazamo tofauti kuhusu usalama wa eneo hilo.
Aidha amesema amemshauri mwakilishi wa Umoja wa Falme za Kiarabu katika kikao cha BRICS kwamba utawala wa Kizayuni na Marekani haviwezi kuwaletea usalama, kama ambavyo sasa wameona athari za kuhifadhi kambi za kijeshi za Marekani.
Araghchi aidha amesisitiza umuhimu wa uhusiano mwema kati ya nchi jirani na ushirikiano wa majirani katika masuala ya usalama badala ya kuwategemea wageni.