Kiongozi Muadhamu: Majeshi ya Iran yawe tayari kukabiliana na adui
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i16258-kiongozi_muadhamu_majeshi_ya_iran_yawe_tayari_kukabiliana_na_adui
Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi yote ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza kuhusu ulazima wa majeshi nchini kujiimarisha kiitikadi, kielimu na kinidhamu sambamba na kuwapa wanajeshi vijana uzoefu wa zama za Kujihami Kutakatifu.
(last modified 2026-02-25T07:04:48+00:00 )
Sep 28, 2016 13:56 UTC
  • Kiongozi Muadhamu: Majeshi ya Iran yawe tayari kukabiliana na adui

Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi yote ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza kuhusu ulazima wa majeshi nchini kujiimarisha kiitikadi, kielimu na kinidhamu sambamba na kuwapa wanajeshi vijana uzoefu wa zama za Kujihami Kutakatifu.

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei, Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi yote ya Iran ameyasema hayo leo katika hafla ya kuhitimu wanachuo wa Chuo Kikuu cha Jeshi la Anga cha Shahid Sattari mjini Tehran. Ameongeza kuwa, Majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran yanapaswa daima kuwa tayari  ili wakati yatakapohitajika yawe tayari kukabiliana ipasavyo na adui.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema, Iran inakabiliana na mrengo mkubwa wa maadui kutokana na msimamo wake wa kuendelea kufungamana na Uislamu, kuwa huru na kuzingatia thamani za juu.

Amesema  zama za Kujihami Kutakatifu ( wakati wa vita vya miaka minane vya kulazimishwa vya Iraq dhidi ya Iran mwaka 1980-1988) zilikuwa zama za mtihani mgumu na kwamba  umahiri wa Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ulibainika kutokana na mafanikio ya jeshi hilo.

Kiongozi Muadhamu akikagua gwaride

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema: "Vita vya kulazimishwa vya miaka minane kwa hakika vilikuwa vita vya kimataifa na hujuma ya pande zote ya madola makubwa  dhidi ya mipaka, utambulisho, thamani, mfumo wa Kiislamu na Mapinduzi ya taifa la Iran.

Ayatullah Khamenei amesema moja ya hatua za dharura katika vyuo vikuu vya majeshi ya Iran ni kuwafahamisha askari vijana kuhusu yaliyojiri katika zama za Kujihami Kutakatifu. Ameongeza kuwa, "Leo dunia nzima, wakiwemo marafiki na maadui, wamekiri kuhusu adhama, ustadi, ushujaa na nguvu za taifa la Iran na mfumo wa Kiislamu. Amiri Jeshi Mkuu pia amepongeza ujasiri, kujitolea muhanga na jihadi ya maafisa wa Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu la Iran.