Iran haitafanya mazungumzo kuhusu uwezo wake wa makombora
Afisa wa ngazi za juu wa kijeshi nchini Iran amesema Jamhuri ya Kiislamu ya Iran haitafanya mazungumzo kuhusu uwezo wake mkubwa wa makombora.
Meja Jenerali Yahya Rahim Safavi, mashauri wa masuala ya kijeshi wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Khamenei amesema: "Marekani inapaswa kufahamu kuwa uwezo wa kijeshi wa Iran na masuala kama ya Syria na Iraq yanayohusiana na usalama wa taifa wa Iran hayawezai kufanyiwa mazungumzo."
Meja Jenerali Safavi ambaye aliwahi kuwa kamanda wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu, IRGC, amesema Wamarekani wanapaswa kuacha uhasama wao wa kisiasa na kusitisha vikwazo vyao vya kidhalimu dhidi ya Iran.
Ameongeza kuwa, kwa mara nyingine matamshi ya Rais wa Marekani Donald Trump yameonyesha hana mtazamo wa kistratijia kuhusu matukio ya kimataifa hasa matukio ya Asia Magharibi.
Aidha amesema Marekani haina uelewa sahihi kuhusu matukio ya Iran huku akitoa wito wa kuwepo tahadhari kuhusu njama za Marekani na vibaraka wake, wakiwemo Wazayuni.