Kiongozi Muadhamu: Marekani ndio utawala fisadi na dhalimu zaidi ulimwenguni
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i38187-kiongozi_muadhamu_marekani_ndio_utawala_fisadi_na_dhalimu_zaidi_ulimwenguni
Ayatullah Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, Marekani ndio utawala fisadi na dhalimu zaidi ulimwenguni.
(last modified 2026-01-14T11:42:18+00:00 )
Dec 27, 2017 15:53 UTC
  • Kiongozi Muadhamu: Marekani ndio utawala fisadi na dhalimu zaidi ulimwenguni

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, Marekani ndio utawala fisadi na dhalimu zaidi ulimwenguni.

Ayatullah Khamenei amesema hayo leo alipoonana na maafisa wa Baraza la Uratibu wa Tablighi ya Kiislamu kote nchini Iran na kuongeza kuwa, Marekani inaendelea kuliunga mkono genge la kigaidi na ukufurishaji la Daesh (ISIS) kwa kushirikiana na tawala wa kidhalimu na kidikteta kama vile Aal Saud. Vile vile amesema, Marekani inaendelea kuunga mkono kwa kila namna jinai za Wazayuni na jinai zinazoendelea kufanywa dhidi ya wananchi wa Yemen na hiyo ni baadhi tu ya mifano ya sura halisi za ufisadi na udhalimu wa utawala wa kibeberu wa Marekani.

Hadhirina wakisikiliza hotuba ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika Husainia ya Imam Khomeini mjini Tehran

 

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amegusia pia ubaguzi wa rangi uliokita mizizi nchini Marekani na katika mfumo wa mahakama wa nchi hiyo na kuongeza kuwa, licha ya mfumo wa mahakama wa Marekani kuwa umeoza kiasi chote hicho lakini nchi hiyo hiyo inavisakama kwa lawama vyombo vya mahakama vya nchi nyingine vikiwemo vyombo vinavyoendeshwa kidini vya mahakama za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.

Ayatullah Khamenei ameongeza kuwa, Marekani inatumia fedha nyingi kuendesha njama tata sana za Marekani kupitia kuzusha mizozo ya kisiasa, kidini, kikaumu na kilugha nchini Iran lakini njama zote hizo zimeshindwa. Ameongeza kuwa, kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu, taifa la Iran na mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu utaikatisha tamaa Marekani katika nyuga zote.

Vile vile amesema, Jamhuri ya Kiislamu itaendelea kupiga hatua za kimaendeleo kwa nguvu zake zote na kusisitiza kuwa: Njia hiyo ya maendeleo itaendelea pia katika kipindi cha rais wa hivi sasa wa Marekani na kwamba maadui wataendelea kuwa na kinyongo cha kushindwa kuitoa Jamhuri ya Kiislamu katika medani au kuidhoofisha.