Apr 22, 2018 13:52 UTC
  • Iran yaalani shambulio la kigaidi Kabul

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amelaani shambulio la kigaidi lililotekelezwa leo huko Kabul mji mkuu wa Afghanistan na kulitaja kuwa ni kitendo cha jinai na kisicho cha kibinadamu.

Kundi la kigaidi la Daesh leo Jumapili lilikishambulia kituo kimoja cha kusajili majina ya wapiga kura huko magharibi mwa Kabul mji mkuu wa Afghanistan. Wizara ya Afya na Tiba ya nchi hiyo imetangaza idadi ya waliopoteza maisha katika shambulio hilo kuwa ni 31 huku majeruhi wakiwa ni 57. 

Bahram Qassemi msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ametoa mkono wa pole kwa serikali na wananchi wa Afghanistan pamoja na familia za wahanga wa hujuma hiyo ya kigaidi na kusema anataraji kuwa kwa irada na juhudi za pamoja katika ngazi zote za pande mbili, kieneo na kimataifa; ugaidi katika miundo yake yote utaangamizwa siku chache zijazo katika eneo hili na ulimwenguni kwa ujumla.  

Bahram Qassemi Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran 

Hilo ni shambulio la tano la kigaidi kutekelezwa katika kituo cha uchaguzi huko Afghanistan katika siku kadhaa za karibuni. Kabla ya shambulio hilo la leo, kundi la Taliban lilikuwa limefanya mashambulizi mengine katika vituo vya majimbo ya Badghis Ghor na Nangarhar nchini humo; mashambulio yaliyosababisha kuuliwa na kujeruhiwa watu kadhaa. Uchaguzi wa bunge na mabaraza ya majimbo  nchini Afghanistan umepangwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu baada ya kuakhirishwa kwa miaka mitatu.  

Tags