Sekta ya mafuta ya Iran inaendelea kustawi licha ya vikwazo vya Marekani
Waziri wa Mafuta wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema sekta ya mafuta na gesi ya taifa hili inaendelea kustawi na kuimarika licha ya vikwazo vya kidhalimu vya Marekani.
Bijan Zangeneh ameyasema hayo leo Jumamosi hapa mjini Tehran na kufafanua kuwa, vikwazo vya Marekani vimeshindwa kuzuia uuzaji wa mafuta ya Iran ya Kiislamu nje ya nchi.
Ameeleza bayana kuwa, "Licha ya vikwazo vya Marekani, lakini treni ya ustawi katika sekta ya mafuta ya Iran haijasitisha mwendo, na huu ni mfano wa wazi wa Uchumi wa Kimuqawama."
Bijan Zangeneh ameyasema hayo katika hafla ya kusainiwa mkataba wa dola milioni 440 kati ya shirika la Petropars na kampuni ya gesi ya Belal.
Kwa mujibu wa mkataba huo, Petropars ambayo ni taasisi iliyoko chini ya Shirika la Taifa la Mafuta la Iran (NIOC) itazalisha mamilioni ya tani ya gesi katika Ghuba ya Uajemi.
Waziri wa Mafuta wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameongeza kuwa, mikataba na miradi zaidi ya sekta ya petrokemikali ya Iran itaendelea kuzinduliwa kadri siku zinavyosonga mbele.