Rouhani: Marekani italipa gharama kubwa ya kumuua shahidi Soleimani
(last modified Sun, 05 Jan 2020 07:50:39 GMT )
Jan 05, 2020 07:50 UTC
  • Rouhani: Marekani italipa gharama kubwa ya kumuua shahidi Soleimani

Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema Marekani itabeba dhima ya matokeo mabaya na radimali za kuuliwa shahidi Luteni Jenerali Qassem Soleimani, aliyekuwa kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi la Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran (SEPAH) na kusisitiza kuwa, Washington italipa gharama kubwa ya ugaidi wake huo.

Rais Hassan Rouhani amesema hayo mjini Tehran katika mazungumzo yake na Mohammed bin Abdulrahman bin Jassim Al Thani, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Qatar na kubainisha kuwa, hapana shaka kuwa, taifa la Iran na mataifa mengine huru katika kanda hii yatalipiza kisasi dhidi ya Marekani mtenda jinai. 

Dakta Rouhani ameongeza kuwa, Washington kwa kutekeleza mauaji hayo ya kigaidi imeamua kukanyaga wazi kanuni zote za kibinadamu na sheria za kimataifa. Amefafanua kuwa, "Marekani imechukua mkondo mpya utakaohatarisha usalama wa eneo, na kwa msingi huo, mashauriano na ushirikiano miongoni mwa nchi marafiki ni jambo la dharura."

Rais Rouhani ameongeza kuwa, anatumai mataifa yote ya eneo hili yatalaani na kushirikiana bega kwa bega kupambana na ugaidi pamoja na kuimarisha umoja na mshikamano wao.

Kwa upande wake, Mohammed bin Abdulrahman bin Jassim Al Thani, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Qatar mbali na kueleza wasiwasi wake kufuatia mauaji hayo ya Soleimani yaliyofanywa kwa amri ya Rais Donald Trump wa Marekani, amesema serikali ya Doha ina hamu ya kuimarisha uhusiano na Tehran katika nyuga mbalimbali.

Zarif alipoonana jana na Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Qatar hapa Tehran

Katika hatua nyingine, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema jinai ya Marekani ya kumuua shahidi Luteni Jenerali Soleimani ni mwanzo wa mwisho wa uwepo wa vikosi ajinabi katika eneo la Asia Magharibi ambavyo ndio sababu ya ukosefu wa amani na usalama na chimbuko la kuongezeka migogoro katika eneo hili.

Dakta Muhammad Javad Zarif aidha ametuma kwenye ukurasa wake wa Twitter picha zinazoonesha mamia ya maelfu ya Wairaqi walivyojitokeza jana kuiaga miili ya mashahidi Soleimani na naibu mkuu wa kikosi cha kujitolea cha wananchi wa Iraq, al Hashdul Shaabi, Abu Mahdi al Muhandes, na kuambatanisha na maneno haya: "Masaa 24 yaliyopita, kikaragosi mwenye kiburi, anayejidai kuwa mwanadiplomasia wa juu wa Marekani (Mike Pompeo), alidai kuwa watu wanashangilia katika miji ya Iraq. Hii leo (jana Jumamosi), malaki ya ndugu zetu Wairaqi wametoa jibu (la upotoshaji huo) kote nchini."

Maelfu ya Wairaqi wakiaga miili ya mashahidi Soleimani na al-Muhandes