Shehena kubwa zaidi ya chanjo ya COVID-19 yaingia Iran
Shehena kubwa zaidi ya chanjo ya COVID-19 imeingia nchini Iran leo ikiwa ni katika jiithada za kuwapa chanjo wananchi wote.
Mohammad Hassan Ghosian Moghaddam Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Hilali Nyekundu ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema jumuiya hiyo ndiyo iliyoingiza shehena hiyo nchini mapema leo.
Katika mahojiano na shirika la habari la IRNA, Ghosian- Muqaddam amedokeza kuwa shehena hiyo yenye dozi milioni moja za chanjo ya COVID-19 kutoka China imeingia nchini Iran kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Imam Khomeini (MA)
Chanjo zingine ambazo zimeruhusiwa kuingia nchini kwa ajili ya matumizi ya dharura ni zile cha Sputnik kutoka Russia, Bharat ya India na Astrazeneca Oxford iliyotegenezwa na shirika la SKBio la Korea Kusini.
Chanjo ya COVID-19 nchini Iran inatolewa kwa mujibu wa Mpango wa Kitaifa wa Chanjo ambao umeidhinishwa na Kamati ya Kitaifa cha Kukabiliana na COVID-19.
Iran iko mbioni kujitegenezea chanjo zake za COVID-19 na inatazamiwa kuwa, baada ya majaribio ya mwisho kwa mwanadamu kukamilika, zitaanza kuzalishwa kwa wingi hivi karibuni.
Wizara ya Afya ya Iran jana ilitangaza kuwa hadi sasa watu 889,095 wamepokea dozi ya kwanza ya COVID-19 na wengine 211,822 wameshapokea dozi ya pili ya chanjo hiyo.
Hadi kufikia jana idadi ya watu ambao walikuwa wameshapoteza maisha hapa nchini kutokana na COVID-19 ilikuwa ni 72,090.