Hatibzadeh: Hakuna "mapatano ya awali" katika mazungumzo ya nyuklia ya Vienna
-
Saeed Khatibzadeh
Msemaji wa Wizara Ya Mambo ya Nchi za Nje ya Iran amesema kuwa, hakuna suala linalotajwa kama "mapatano ya awali" katika mazungumzo ya nyuklia yanayoendelea huko Vienna, Austria, na kwamba asilimia kubwa ya masuala yaliyobaki yamekamilishwa kna yanasubiri maamuzi ya kisiasa.
Saeed Khatibzadeh amewaambia waandishi wa habari leo mjini Tehran kwamba, hakuna suala la mapatano ya awali katika mazungumzo ya nyuklia ya 4+1, na mapatano hayatafikiwa baina ya pande mbili ila baada ya mambo yote kutatuliwa.
Akijibu madai ya kituo cha habari cha Middle East Eye chenye makao yake nchini Uingereza kwamba, katika mazungumzo yake na Saudi Arabia, Iran imeomba msaada wa kupata njia ya kuuza mafuta na kupiga chenga vikwao vya Marekani, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje ya Iran amesema kuwa, hayo ni madai yasiyo na msingi na ya uongo. Amesema, mazungumzo ya Iran an Saudia yanahusu masuala ya pande mbili, ya kikanda na kimataifa, na madai kama hayo hayana msingi wowote.
Katika sehemu nyingine ya matamshi yake mbele ya waandishi wa habari, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje ya Iran amesema kuwa, thamani na mapambano ya ukombozi wa Palestina ni masuala muhimu ya mataifa ya Waislamu kwa miongo kadhaa sasa. Amesema Iran inaipa kipaumbele kadhia ya Palestina katika siasa zake za nje. Ameongeza kuwa baadhi ya nchi za Kiarabu zilifanya mchezo wa kuigiza wa kuanzisha uhusiano na utawala wa kizayuni wa Israel kwa shabaha ya kuwasahaulisha walimwengu kadhia nambari moja ya Umma wa Kiislamu yaani kadhia ya Palestina, lakini zilisahau kwamba, hakuna jambo linaloweza kuwasaulisha Waislamu umuhimu wa kadhia hiyo.
Amesema kuwa Jamhuri ya Kiislamu imeanzisha harakati za kidiplomasia na mashauriano na nchi za Kiislamu kuhusu hali ya sasa ya Palestina na kwamba, hotuba iliyotolewa jana na Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Muhamamd Javad Zarif katika kikkao cha dharura cha Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu (OIC) imeashiria masuala kadhaa katika uwanja huo ikiwa ni pamoja na kutaka kutambuliwa jinai zinazofanywa na Israel huko Palestina kuwa ni jinai za kivita na jinai dhidi ya binadamu.