Yemen yatetea jibu la kijeshi la Iran kwa utawala wa Kizayuni
Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Serikali ya Uokovuwa Kitaifa ya Yemen imetaja hatua ya Iran ya kuvurumisha makombora na ndege zisizo na rubani (drone) katika kujibu mashambulizi ya utawala wa Kizayuni wa Israel katika sehemu ya ubalozi mdogo wa Jamhuri ya Kiislamu huko Damascus, Syria kuwa ni jibu halali na lililotekelezwa kwa mujibu wa sheria za kimataifa.
Baada ya shambulio la utawala wa Kizayuni unaotekeleza mauaji ya kimbari dhidi ya Wapalestina huko Ukanda wa Gaza la tarehe 1 Aprili katika sehemu ya ubalozi mdogo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran mjini Damascus Syria lilowauwa shahidi washauri saba wa kijeshi wa nchi hii huku jamii ya kimataifa ikinyamaza kimya bila ya kutoa tamko lolote la wazi la kulaani jinai hiyo ya Israel, asubuhi ya jana Jumapili Aprili 14 Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu lilichukua hatua ya kuuadhibu utawala huo vamizi kwa kuvurumisha ndege zisizo na rubani na makombora kadhaa kuelekea maeneo yanayokaliwa kwa mabavu.
Naye Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Umoja wa Mataifa amesema kuwa Iran imetekeleza hatua hiyo ya kijeshi kwa mujibu wa kifungu cha 51 cha Hati ya Umoja wa Mataifa kuhusu kujilinda kihalali na katika kujibu hujuma ya utawala wa Kizayuni katika maeneo ya kidiplomasia ya Iran huko Damascus.
Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Serikali ya Uokovu wa Kitaifa ya Yemen imesisitiza katika taarifa yake kuwa: Jibu la kijeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa utawala wa Kizayuni ni la kisheria na linakwenda sambamba na sheria za kimataifa na Hati ya Umoja wa Mataifa; kwa sababu liko katika kalibu ya haki ya kujilinda.