UNICEF: Watoto milioni 87 duniani wanajua vita tu
https://parstoday.ir/sw/news/uncategorised-i3787-unicef_watoto_milioni_87_duniani_wanajua_vita_tu
Zaidi ya watoto milioni 86.7 wa chini ya umri wa miaka saba wameishi maisha yao yote katika maeneo ya vita na kuhatarisha ukuaji wa ubongo wao.
(last modified 2023-11-27T12:14:11+00:00 )
Mar 25, 2016 15:52 UTC
  • UNICEF: Watoto milioni 87 duniani wanajua vita tu

Zaidi ya watoto milioni 86.7 wa chini ya umri wa miaka saba wameishi maisha yao yote katika maeneo ya vita na kuhatarisha ukuaji wa ubongo wao.

Hayo ni kwa mujibu wa ripoti mpya ya Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF. Ripoti hiyo imeongeza kuwa katika miaka saba ya mwanzo ya maisha ya mtoto ubongo wake huwa una uwezo wa kuamsha seli 1,000 za ubongo kila sekunde. Kila moja ya seli hizo ziitwazo neva zina uwezo wa kuungana na neva zingine 10,000 kwa sekunde. Na ubongo ndio muhimili wa mustakabali wa mtoto katika kutanabahi afya zao, jinsi wanavyohisi na uwezo wa kujifunza.

Kwa mujibu wa UNICEF watoto wanaoishi kwenye vita mara nyingi wanashuhudia ukatili uliokithiri, na hivyo kuwaweka katika hatari ya maisha yaliyogubikwa na msongo wa mawazo, hali ambayo huzuia uhusiano muhimu wa neva katika ubongo na kuleta madhara makubwa ya maisha kwa maendeleo yao ya utambuzi, kijamii na kimwili.

Mbali ya athari hizo za kimwili UNICEF inasema pia kuna hatari ya watoto kuathirika kihisia.

Takwimu zinaonyesha kwamba mtoto mmoja kati ya 11 wenye umri wa miaka sita au chini ya hapo wametumia muda muhimu wa ukuaji wa ubongo wao katika vita.

Bara la Afrika ni kati ya maeneo yanayokumbwa na vita duniani huku migogoro ikizidi kutokota katika nchi kama vile Sudan Kusini, Somalia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Jamhuri ya Afrika ya Kati na Nigeria.