Kan TV: Askari 17 wa Israel wameuawa katika mashambulizi ya Hizbullah
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i109742-kan_tv_askari_17_wa_israel_wameuawa_katika_mashambulizi_ya_hizbullah
Vyombo vya habari vya Kizayuni vimetangaza kuwa, wanajeshi 17 wa utawala wa haramu wa Israel wameangamizwa katika mashambulizi ya Harakati ya Hizbullah ya Lebanon.
(last modified 2024-03-21T06:42:30+00:00 )
Mar 21, 2024 06:42 UTC
  • Kan TV: Askari 17 wa Israel wameuawa katika mashambulizi ya Hizbullah

Vyombo vya habari vya Kizayuni vimetangaza kuwa, wanajeshi 17 wa utawala wa haramu wa Israel wameangamizwa katika mashambulizi ya Harakati ya Hizbullah ya Lebanon.

Shirika la habari la Palestina la Sama limenukuu ripoti ya kanali ya Kan TV inayofadhiliwa na Tel Aviv inayosema kuwa, askari 17 wa Kizayuni wameuawa katika hujuma za makombora na maroketi za Hizbullah tokea Oktoba 7, 2023 hadi sasa.

Ripoti hiyo ambayo haijathibitishwa au kukanushwa na jeshi la Israel imeongeza kuwa, takriban makombora na maroketi 3,500 yamevurumishwa na Hizbullah kutoka Lebanon na 38 kutoka Syria na kupiga kaskazini mwa ardhi ya Palestina inayokaliwa kwa mabavu na kupachikwa jina bandia la Israel.

Muqawama wa Kiislamu wa Lebanon kwa miezi kadhaa sasa umeendelea kupiga kwa makombora kambi za kijeshi na maeneo mengine ya Wazayuni huko kaskazini mwa Palestina yaliyopachikwa jinai bandia la Israel.

Jana usiku pia, Harakati ya Hizbullah ya Lebanon ilijibu jinai za utawala wa Kizayuni dhidi ya Ukanda wa Gaza kwa kukivurumishia makombora kituo cha jeshi la Israel katika maeneo ya kaskazini. Aidha wanamuqawama wa Hizbullah jana walishambulia kwa kombora gari la deraya la Israel katika eneo la Al-Baghdadi, mpakani na Lebanon.

Wakati huo huo, Jenerali Tamir Hayman, mkuu wa zamani wa idara ya ujasusi ya jeshi la utawala haramu wa Israel amesema walowezi 80,000 wa Kiyahudi wamelazika kuyakimbia makazi yao katika maeneo ya kaskazini, baada ya kutiwa wahaka na hujuma za makombora ya Hizbullah.

Hizbullah ya Lebanon imesisitiza kuwa, harakati hiyo ya muqawama inafanya mashambulizi yake dhidi ya Wazayuni kujibu mashambulio ya utawala wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina wa Gaza, na kwamba uungaji mkono wa kivitendo wa Hizbullah kwa wakazi wa Gaza utaendelea.