Sayyid Nasrallah asema Rais Raisi alikuwa mujahid
Katibu Mkuu wa Harakati ya Muqawama ya Hizbullah ya Lebanon ametuma salamu za rambirambi kufuatia kufa shahidi Rais wa Iran Sayyid Ebrahim Raisi na Waziri wa Mambo ya Nje Hossein Amir-Abdollahian na ujumbe walioandamana nao.
Sayyid Hassan Nasrallah ametuma salamu za rambirambi kwa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Sayyid Ali Khamenei, viongozi na wananchi wa Iran kufuatia kufa shahidi Rais Raisi na wenzake.
Katika ujumbe huo uliotumkwa kwa Kiongozi kwa niaba ya Hizbullah, wapiganaji wake wa muqawama, familia za mashahidi wake na waliojeruhiwa, na wafuasi wa muqawama, Sayyid Nasrallah amesema, "Tuko pamoja katika masikitiko ya kupoteza viongozi hawa waheshimiwa katika hatua hii nyeti unapoliongoza taifa la Kiislamu katika mapambano yake makali dhidi ya madolea ya kiistikbari na kibeberu.”
Kiongozi wa Hizbulla amesema shahidi Rais Raisi alikuwa "Mujahid (anayepigana kwenye njia ya Mwenyezi Mungu) na mtumishi mwaminifu," na waziri wake wa mambo ya nje, Hossein Amir-Abdollahian, "aliyebeba bendera ya kutetea muqawama katika majukwaa yote ya kimataifa."
"Kwetu sisi, na kwa wote wanaodhulumiwa, wapiganaji wa muqawama, na wapiganaji katika njia ya haki, tunatoa rambirambi zetu na tuna matumaini kuhusu uwepo wako wenye baraka na uongozi wenye hekima na busara." Nasrallah ameongeza.
Ameendelea kusema kuwa: “Namuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu akurefushie umri wako mtukufu na autie nguvu moyo wako safi ili uweze kubeba machungu ya kuwapoteza viongozi hawa waaminifu na watiifu, na azijaalie subira, faraja na malipo makubwa familia zao tukufu, Wairani wetu wapenzi na viongozi wote watukufu wa Jamhuri ya Kiislamu, Mungu akipenda."