Mfamle wa Saudia awapa 'bonasi' askari wanaoua raia Yemen
Mfalme wa Saudi Arabia ametangaza kuwapa marupurupu askari vamizi wanaotekeleza mauaji na jinai za kutisha dhidi ya raia wa kawaida nchini Yemen.
Mfalme Salman bin Abdulaziz Aal-Saud amepasisha dikrii iliyoagiza wanajeshi hao wa Saudia wapewe kifutajasho au marupurupu, kiasi sawa na mshahara wao wa mwezi mmoja kutokana na 'kazi ngumu' wanayoifanya nchini Yemen.
Aidha malipo hayo ya ziada watapewa maafisa katika wizara za usalama, intelijensia, mambo ya ndani pamoja na Gadi ya Taifa, kwa kufanikisha operesheni hizo za kivamizi dhidi ya taifa la Yemen.
Dikrii hii imetolewa siku chache baada ya Sheikh Abdul Aziz Aal ash-Sheikh, Mufti Mkuu na mwanazuoni mashuhuri wa Saudia kutoa fatwa na kusema kuwa ni 'jukumu takatifu na la kiroho' kwa kila Mwislamu nchini humo kutoa 'sadaka' na kuchangia kwa ajili ya kufanikisha operesheni za askari wa Aal-Saud wanaofanya mashambulizi nchini Yemen.
Alisema askari hao wanahitajia msaada wa kifedha haswa wanaofanya hujuma hizo katika maeneo ya mpakani ya Najran, Asir na Jizan.
Mashambulizi ya anga ya jeshi la utawala huo dhidi ya Yemen yaliyoanza Machi mwaka jana, yamesababisha vifo vya watu zaidi ya 10,000 hadi sasa wakiwemo watoto karibu 2,000.