Hizbullah: Tulikwamisha askari 75,000 wa Israel kusini mwa Lebanon
Katibu Mkuu wa Harakati ya Muqawama ya Hizbullah, Sheikh Naim Qassem amesema wanamapambano wa Muqawama waliwazuia askari 75,000 wa jeshi la adui Mzayuni kusonga mbele kusini mwa Lebanon wakati wa vita vya karibuni zaidi.
Katika ujumbe kwa maveterani na majeruhi wa vita wa Hizbullah jana Jumamosi, Sheikh Qassem alisema, "Ummah wa Kiislamu unakabiliwa na mapambano makubwa yanayoongozwa na Twaghut wa Marekani pamoja na nchi zingine za Magharibi, na uchokozi wa kikatili wa utawala wa Kizayuni."
Sheikh Qassem ameeleza kwamba, katika vita vya hivi karibuni kabla ya kusitishwa mapigano, "Wapiganaji wa Muqawama waliwarejesha nyuma wanajeshi maadui 75,000 wa Israel katika mipaka ya kusini mwa Lebanon."
Kiongozi huyo wa kidini na kisiasa wa Lebanon ameeleza bayana kuwa, baada ya wanamuqawama kuwakwamisha askari makatili wa Kizayuni, wananchi wa Lebanon walirudi katika ardhi yao mara tu baada ya kutangazwa kwa kusitisha mapigano ili kuilinda kwa maisha yao, imani, na azma yao.
Akiwahutu wapiganaji wa Muqawama, Sheikh Qassem amesema: "Mapmabano yenu katika vita yalizuia upanuzi wa unyakuzi wa ardhi nchini Lebanon na kuzuia mpango uliowekwa na Marekani kwa ajili ya 'Mashariki ya Kati Kubwa.'
Amebainisha kuwa, "Kwa Muqawama huu, ardhi itabaki kwa ajili ya watu wake na nchi kwa ajili ya watoto wake. Bila kujali shinikizo na maelewano, mlingano wa nguvu utabadilika kwa maslahi ya Muqawama."
Katibu Mkuu wa Harakati ya Muqawama ya Hizbullah amemalizia kwa kusema: Tunawaenzi maveterani mashujaa, hasa maveterani wa mashambulizi ya Pager. Tunawapongeza ndugu na familia zao waliowaunga mkono na kusimama nao. Tunawaenzi wale waliowapokea na kuwapa msaada, na tunamsalimu Imam Khamenei, Kiongozi na Kamanda wa njia na harakati hii takatifu.”