Netanyahu aahirisha kikao cha kuidhinisha ujenzi mpya wa vitongoji Quds Mashariki
Viongozi wa utawala ghasibu wa Kizayunii wametangaza habari ya kuakhirishwa upigaji kura wa kuidhinisha mpango wa kuruhusu ujenzi wa nyumba mpya 500 za walowezi wa Kizayuni huko mashariki mwa Baitul Muqaddas.
Hanan Rubin Mjumbe wa Kamati ya Makazi na Mipango huko Baitul Muqaddas jana Jumatano alisema kuwa kikao cha upigaji kura cha utawala huo kimeakhirishwa kufuatia ombi la Benjamin Netanyahu Waziri Mkuu wa utawala huo wa Tel Aviv. Rubin amesema kuwa Netanyahu amewasilisha ombi hilo ili kuepuka kuzuka mivutano zaidi katika uhusiano kati ya Tel Aviv na Washington.
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa tarehe 23 mwezi huu liliidhinisha azimio nambari 2334 la kulaani ujenzi wa vitongoji unaofanywa na Israel katika maeneo ya Palestina kwa kura 14 za ndio. Marekani pekee ndiyo ilijizuia kulipigia kura azimio hilo.
Kwa mujibu wa azimio hilo, utawala wa Kizayuni unanapasa kusimamisha kikamilifu ujenzi wa nyumba za walowezi wa Kiyahudi katika maeneo ya Palestina, ikiwemo Quds Mashariki. Utawala wa Kizayuni ulitangaza baada ya kupasishwa azimio hilo kuwa hautalitekeleza. Hatua ya Marekani nchi ambayo inajulikana kama muitifaki mkuu wa utawala wa Kizayuni ya kutolipigia veto azimio hilo la Baraza la Usalama, imewakasirisha viongozi wa Kizayuni.