Jihadul Islami: Saudia na Imarati zinashirikiana na Marekani kuikandamiza Palestina
Mwakilishi wa harakati ya Jihad al Islami ya Palestina nchini Iran amesema kuwa, Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu (Imarati), zinashiriki waziwazi katika 'Mapatano ya Karne' ambayo yameandaliwa na Marekani na utawala wa Kizayuni wa Israel kuliangamiza taifa la Palestina
Shirika la habari la IRIB limemnukuu Nasser Abu Sharif akisema hayo jana Jumatano katika kikao maalumu kilichofanyika hapa Tehran na kuongeza kuwa, Marekani, utawala wa Kizayuni wa Israel na baadhi ya watawala wa nchi za Kiarabu wa eneo hili wanawashinikiza Wapalestina waachane na malengo yao muhimu na matukufu kama vile haki ya kurejea wakimbizi wa Kipalestina katika ardhi zao.

Ameongeza kuwa, muqawama na Intifadha ya Palestina katika miongo kadhaa iliyopita imethibitisha kuwa taifa la Palestina haliko tayari kuachana na malengo yake matakatifu kwa hali yoyote ile.
'Mapatano ya Karne' ni mpango mpya wa serikali ya Marekani wenye lengo la kuangamiza kikamilifu haki za wananchi wa Palestina.
Kwa mujibu wa mpango huo, mji mtakatifu wa Quds utakabidhiwa kikamilifu mikononi mwa utawala wa Kizayuni, wakimbizi wa Kipalestina walioko katika nchi nyingine hawatakuwa na haki ya kurejea Palestina, na ardhi pekee itakayobakia mikononi mwa Palestina ni Ukanda wa Ghaza na eneo ilipo Mamlaka ya Ndani ya Palestina katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.