Msemaji wa Hamas: Mapambano ndiyo njia pekee ya kuikomboa Palestina
(last modified Tue, 10 Dec 2019 13:19:56 GMT )
Dec 10, 2019 13:19 UTC
  • Intifadha ya Wapalestina
    Intifadha ya Wapalestina

Msemaji wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (HAMAS) amesema kuwa, mapambano ya pande zote na kwa kutumia mbinu na nyezo zote ndiyo chaguo la taifa la Palestina kwa ajili ya kukabiliana na utawala ghasibu wa Israel.

Abdullatif al-Qanou amesema katika maadhimisho ya mwaka wa 32 wa kuanza Intifadha ya kwanza ya Wapalestina iliyopewa jina la Intifadha ya Jiwe kwamba mapambano ya Intifadha yamehuisha moyo wa kujitolea wa taifa la Palestina kwa ajili ya kukabiliana na Wazayuni maghasibu.

Al Qanou amesisitiza udharura wa kuendelezwa mapambano ya ukombozi wa Palestina ya Intifadha na kusema kuwa, maandamano ya Haki ya Kurejea yanayofanywa kila siku ya Ijumaa ya Wapalestina wa Ukanda wa Gaza na kuvunjwa mzingiro wa Israel dhidi ya wakazi wa eneo hilo ni baadhi ya nyenzo zinazotumiwa na Wapalestina katika mapambano yao dhidi ya utawala haramu wa Israel.

Intifadha ya Jiwe

Intifadha ya Kwanza au Intifadha ya Jiwe ilianza tarehe 9 Disemba mwaka 1987 katika kambi ya wakimbizi ya Jabalia huko kaskazini mwa Ukanda wa Gaza na kupanuka zaidi katika miji na maeneo mengine ya Palestina. Katika mapambano hayo ya Intifadha ya Kwanza yaliyoendelea kwa kipindi cha miaka 6, Wapalestina 1300 waliuawa shahidi kwa kipigwa risasi na askari wa utawala haramu wa Israel.