Baraza la Usalama latakiwa kusaidia kurejesha amani nchini Yemen
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i79106-baraza_la_usalama_latakiwa_kusaidia_kurejesha_amani_nchini_yemen
Mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Yemen amelitaka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuunga mkono na kusaidia juhudi za kurejesha amani na uthabiti nchini Yemen.
(last modified 2026-08-11T03:40:48+00:00 )
Jan 12, 2022 04:44 UTC
  • Baraza la Usalama latakiwa kusaidia kurejesha amani nchini Yemen

Mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Yemen amelitaka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuunga mkono na kusaidia juhudi za kurejesha amani na uthabiti nchini Yemen.

Hans Grundberg  amesema hayo akiwa nchini Uingereza katika mazungumzo yake na viongozi na maafisa wa ngazi za juu wa serikali ya London ambapo amebainisha kwamba, kwa sasa Yemen inakabiliwa na hali mbaya ya kiuchumi sambamba na kuongezea vita na mapigano katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo.

Akizungumza mwishoni mwa safari yake nchini Uingereza, mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Yemen amesema kuwa, kushadidi mizozo ya kijeshi hakuwezi kupelekea kupatikana kwa njia za kudumu za ufumbuzi.

Afisa huyu wa Umoja wa Mataifa ameeleza kuwa, pande zinazozana nchini Yemen zinaweza na zinapaswa kushiriki katika mazungumzo ya kisiasa kwa minajili ya kumaliza hitilafu na hivyo kupatikana ufumbuzi jumuishi kupitia mazungumzo.

 

Aidha amesema kuwa, daima Umoja wa Mataifa umekuwa tayari na una shauku ya kuunga mkono mwenendo na mchakato wa mazungumzo baina ya pande hasimu nchini Yemen.

Kadhalika amesisitiza kuwa, himaya na uungaji mkono wa jamii ya kimataifa na nchi wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ni jambo la dharura kwa ajili ya kupata mafanikio na kufikia lengo hilo.

Hayo yanaripotiwa katiika hali ambayo, katika siku za hivi karibuni mashambulio ya anga ya muungano vamizi unaoongozwa na Saudi Arabia yameshadidi mno katika maeneo mbalimbali ya Yemen ukiwemo mji mkuu Sana'a.