Venezuela: Watu 200 waliuawa, kujeruhiwa wakati wa kutekwa Maduro
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Venezuela amesema idadi ya watu waliouawa na kujeruhiwa katika shambulio la karibuni la Marekani wakati ikimteka nyara Rais Nicolas Maduro wa nchi hiyo ya Amerika ya Latini imeongezeka na kupindukia watu 200.
Diosdado Cabello, Waziri wa Mambo ya Ndani wa Venezuela amesema hayo katika kikao na waandishi wa habari mjini Caracas na kueleza kuwa: Kufikia sasa watu 100 wamepoteza maisha na wengine zaidi ya 100 wamejeruhiwa.
Amesema, "Shambulio hilo lilikuwa la kuogofya. Ni ukweli mchungu ambao hauwezi kufichika. Hata wanawake waliokuwa katika majumba yao walishambuliwa na kujeruhiwa wakati wa hujuma hiyo ya kivamizi ya Januari 3.
Wanajeshi wa Marekani walimteka nyara Maduro na mkewe Cilia Flores na kuwasafirisha hadi Marekani kwa ajili ya kushtakiwa kwa madai ya magendo ya mihadarati, kula njama, kuingiza kokaini nchini Marekani na magendo ya silaha.
Maduro ambaye kwa muda mrefu amekanusha madai hayo, hivi karibuni aliiambia mahakama mjini New York kwamba yeye ni mateka wa vita na kukana mashtaka yanayohusiana na dawa za kulevya. Umoja wa Mataifa umetangaza kuwa, operesheni ya kijeshi ya Marekani nchini Venezuela ilikuwa ukiukaji wa sheria za kimataifa.
Ravina Shamsadani, Msemaji Mkuu wa Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa (OHCHR) amesema mashambulizi ya Marekani dhidi ya Venezuela yanadhoofisha kanuni ya msingi ya sheria za kimataifa.