Viongozi wa Myanmar wazuia uchunguzi kuhusu jinai dhidi ya Waislamu
Viongozi wa serikali ya Myanmar wamewazuia waandishi wa habari na waangalizi wa asasi kadhaa za kimataifa kufanya safari katika mkoa wa Rakhine ambao kwa miezi kadhaa umeshuhudia machafuko na ukatili mkubwa dhidi ya jamii ya Waislamu wa nchi hiyo.
Hii ni katika hali ambayo askari usalama wa Myanmar wanatuhumiwa kuhusika moja kwa moja katika jinai dhidi ya Waislamu wa mkoa huo na ripoti kuhusiana na suala hilo imepangwa kutangazwa hivi karibuni kupitia kamisheni ya uchunguzi ambayo iliundwa na serikali kwa ajili ya shughuli hiyo. Hata hivyo baada ya timu ya waandishi wa habari kuwasili katika mkoa wa Rakhine, viongozi wa eneo hilo waliwaambia kuwa, hakutakuwa na safari kuelekea maeneo yaliyokumbwa na machafuko hayo.
Hivi karibuni kulisambaa picha za ukatili wa kijinsia unaowahusisha askari wa Myanmar wakiwabaka makumi ya wanawake wa Kiislamu wa mkoa huo na kadhalika picha za makumi ya miili ya Waislamu waliouawa na askari hao. Ukatili huo ulikuwa mkubwa kiasi cha kuwafanya hata baadhi ya askari kushindwa kuvumilia na hivyo kuamua kueneza video na picha zinazoonyesha askari hao wakipiga na kuwanajisi wanawake wa Kiislamu wa kabila la Rohingya.
Kufuatia hali hiyo na kutokana na mashinikizo mbalimbali ya jamii ya kimataifa, hatimaye serikali ya Naypyidaw iliamua kuunda kamati ya uchunguzi ambayo ilitakiwa kuwasilisha ripoti yake mwishoni mwa mwezi huu wa Januari. Weledi wa mambo wameitaja hatua ya serikali ya nchi hiyo ya kuunda kamati hiyo kuwa ni kujaribu kujisafisha na ukatili wa askari hao.
Kwa mujibu wa duru za habari mashambulizi ya hivi karibuni ya Mabudha dhidi ya Waislamu hao kwa akali yemepelekea watu elfu 66 wa kabila la Rohingya kukimbilia usalama wao nchini Bangladesh.