Russia yatahadharisha kuhusu njama mpya ya silaha za kemikali Syria
Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Russia imetahadharisha kuhusu uwezekano wa kutokea mashambulizi mapya ya silaha za kemikali nchini Syria kwa shabaha ya kuituhumu serikali ya Damascus na baadaye kuishambulia nchi hiyo.
Taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Russia imetahadharisha kwamba, kuna njama ya kufanyika mashambulizi ya silaha za kemikali nchini Syria kwa lengo la kutoa pigo kwa serikali ya nchi hiyo.
Msemaji wa wizara hiyo, Maria Zakharova amesema kuwa, kuna harakati mpya za kufanya mashambulizi ya silaha za kemikali nchini Syria ambayo lengo lake ni kuituhumu serikali ya Damascus kuwa ndiyo iliyofanya mashambulizi hayo.
Zakharova ameongeza kuwa, inatabiriwa kuwa katika duru ya sasa pia kutatolewa madai ya kuhusika serikali ya Syria na mashambulizi ya silaha za kemikali dhidi ya raia.
Katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita nchi za Magharibi zikiongozwa na Marekani zimekuwa zikiituhumu serikali ya Damascus kuwa imetumia silaha za kemikali dhidi ya raia wake katika maeneo kama Khan Shaykhun na Ghouta Mashariki, na zimeshambulia vituo vya serikali ya nchi hiyo kwa kutegemea madai hayo ambayo hayakudhibitishwa.