Watu zaidi ya 32 wauawa katika hujuma msikitini Qandahar, Afghanistan
Hujuma ya kigaidi imelenga msikiti wa Waislamu wa madhehebu ya Shia katika mji wa Kandahar, Afghanistan na kuepelekea waumini wasiopungua 32 kuuawa shahidi na wengine zaidi ya 53 kujeruhiwa.
Kwa mujibu wa taarifa, hujuma hiyo imejiri leo adhuhuru wakati wa Swala ya Ijumaa katika Msikiti wa Bibi Fatima katika mji wa Kandahar. Walioshuhudia wanasema kumejiri milipuko miwili, mmoja katika mlango na mwingine ndani ya msikiti huo wakati wa Sala ya Ijumaa.
Hadi sasa hakuna kundi lolote ambalo limedai kuhusika na hujuma hiyo ingawa wiki iliyopita magaidi wakufurishaji wa ISIS au Daesh walidai kuhusika na hujuma dhidi ya msikiti mwingine wa Mashia mjini Kunduz ambapo waumini karibu 80 waliuawa shahidi wakati wa Swala ya Ijumaa.

Msemaji wa serikali ya Taliban Zabihulla Mujahid amesema maafisa wa serikali wametoa amri ya kukamatwa na kufikishwa kizimbani wahusika wa hujuma ya leo mjini Qandahar.