Iran: Filihali sio muda mwafaka wa kufanya mazungumzo na Marekani
-
Iran: Filihali sio muda mwafaka wa kufanya mazungumzo na Marekani
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, kwa sasa sio muda mwafaka wa kufanya mazungumzo na Marekani.
Seyyed Abbas Araghchi, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran jana Jumatano aliwaambia waandishi wa habari akijibu swali kuhusu hali na mchakato wa mazungumzo kati ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Marekani: "Sasa si wakati mwafaka wa mazungumzo, na hii ni kwa sababu ya sera za Washington DC".
Araghchi aliongeza: "Jamhuri ya Kiislamu ya Iran haijawahi kuondoka kwenye meza ya mazungumzo. Siku zote tumekuwa tayari kwa mazungumzo yenye msingi na heshima ya pande zote mbili, lakini serikali ya Marekani haina utendaji kama huo kwa sasa." Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, huku akisisitiza juhudi za kuondoa vikwazo vya kidhalimu vya Magharibi, hasa Marekani, aliongeza: "Tunafanya juhudi kubwa za kuendeleza uhusiano wa kibiashara na ushirikiano wa kiuchumi na majirani zetu.
Hivi karibuni pia Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran alinukuliwa akisema kuwa, Tehran itaendelea kuwa muwazi kuhusu mazungumzo, na msimamo wake utaendelea kuwa ule ule kwamba mazungumzo maana yake ni mazungumzo, si udikteta. Inaweza kufikiria kufanya mazungumzo na Marekani, lakini tu ikiwa Washington itabadilika na kuacha madai yake yasiyo na mantiki. Iingie kwenye mazungumzo ya kuheshimiana na ya usawa si ya kufanyiana udikteta.